Shukrani hizo zimetolewa na Mkurugenzi Msaidizi wa Ufuatiliaji Haki kutoka Wizara ya Katiba na Sheria, Lawrence Kabigi, aliyeongoza masafara wa watumishi wa kituo hicho, wafanyakazi wa MoCLA na Wanasheria wa Serikali, alipokuwa akitoa neno la shukrani kwa Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB, Bi. Ruth Zaipuna baada ya kukamilisha mafunzo yao.
Kabigi alibainisha kuwa, siku mbili za mafunzo yao NMB, hususani katika Kituo cha Huduma kwa Wateja ‘NMB Contact Center,’ yeye na washiriki wengine kutoka MoCLA wamejifunza mengi, ikiwemo namna kituo hicho na taasisi nzima inavyotoa huduma tangu kupokea malalamiko na kero za wateja wao na kuyashughulikia kwa utaratibu wa kisasa zaidi.
“Tulikuja hapa pia kuona tunatofautiana vipi katika teknolojia kwenye kushughulikia changamoto za wateja wenu, tumejionea namna mlivyotengeneza mifumo bora, sahihi na ya kisasa inayoshughulikia changamoto. Mifumo mizuri ambayo haimhitaji tu mfanyakazi kujibu, bali mifumo yenyewe inajibu na kuleta suluhishi za kimahitaji.
“Na sisi tunaangalia namna ya kufikia ufanisi wenu katika kuhudumia wananchi wanaosubiri kutoka kwetu ufumbuzi wa changamoto zao, tukiamini kwamba tunapopambana kumaliza kero na changamoto za wananchi bila kutumia muda wao, tuNawapa wigo mpana wa kuendelea kuwajibika na uzalishaji mwingine na kukuza pato lao na la taifa kwa ujumla.
“Mwananchi ambaye tutamsaidia kumaliza changamoto zake, hata asipotulipa tutakuwa tumempa muda wa kufanya mambo mengine na kwa mantiki hiyo ataweza kulipa kodi serikalini.
“Kimsingi sisi hatubagui malalamiko ya wananchi, tunayapokea yote na yaliyo ndani ya wizara yetu yanatatuliwa, na yale ya wizara ama idara za serikali, taasisi za umma na binafsi tunayapeleka na tunafuatilia ufumbuzi wake.
“Tunashukuru kwa mafunzo haya, ambayo si tu yalikuwa ya nadharia, bali kwa vitendo kupitia wataalam mahiri na wabobevu wanaohudumu kwenye vitengo mbalimbali bila kuathiri usiri wa taarifa za wateja wenu,” alisema Kabigi na kutaka mashirikiano baina ya MoCLA yaendelee kwa ustawi wa maisha ya Watanzania wa kada zote.






















































