Dar es Salaam, Agosti 20, 2026: Vodacom Tanzania Plc imeendelea kuonyesha ukuaji imara na kuongeza thamani kwa wanahisa, wateja na jamii katika mwaka wa fedha ulioishia Machi 31, 2026, huku uwekezaji katika miundombinu ya mawasiliano, huduma za kidijitali na huduma jumuishi za kifedha ukiendelea kuwa kichocheo muhimu cha mafanikio hayo.
Matokeo hayo yalitangazwa wakati wa Mkutano Mkuu wa 10 wa Mwaka wa Wanahisa wa Vodacom Tanzania Plc, ambapo wanahisa walijadili na kuidhinisha maazimio mbalimbali yanayohusu utendaji wa Kampuni, malipo ya gawio, muundo wa Bodi, utawala bora na mwelekeo wa biashara kwa siku zijazo.
MAPATO YA HUDUMA YAFIKIA TZS 1.8 TRILIONI
Katika mwaka wa fedha 2026, mapato ya huduma ya Vodacom Tanzania yaliongezeka kwa 21.8% hadi kufikia TZS 1.8 trilioni, huku EBITDA ikiongezeka kwa 38.8% hadi TZS 684.9 bilioni.
Faida baada ya kodi ilifikia TZS 107.1 bilioni, ikiwakilisha ongezeko la 18.4% ikilinganishwa na mwaka uliotangulia.
Wakati huo huo, idadi ya wateja iliongezeka kwa 22.3% hadi kufikia milioni 27.7, ikichangiwa na ongezeko la 22.5% la wateja wa intaneti na 22.6% la wateja wa M-Pesa.
UWEKEZAJI WA TZS 323.9 BILIONI KATIKA MTANDAO
Utendaji huo umechangiwa kwa kiasi kikubwa na uwekezaji mkubwa katika mtandao, teknolojia na majukwaa ya kidijitali.
Uwekezaji wa mitaji (CAPEX) uliongezeka kwa 85.1% hadi kufikia TZS 323.9 bilioni, ukiwezesha Kampuni kuongeza vituo vipya 444 vya 4G na 25 vya 5G, sambamba na kuimarisha mifumo ya TEHAMA na mtandao kwa ujumla.
Kutokana na uwekezaji huo, wigo wa mtandao wa 4G ulifikia 76.3%, ikiwa ni ongezeko la asilimia 3.8, huku idadi ya watumiaji wa simu janja ikiongezeka kwa 31.5%.
Tangu mwaka 2013, Vodacom Tanzania imejenga pia vituo 466 katika maeneo ya vijijini kupitia mpango wa Serikali wa kuimarisha upatikanaji wa huduma za mawasiliano vijijini.
WANAHISA KUPATA GAWIO LA TZS 53.6 BILIONI
Utendaji mzuri wa Kampuni umewezesha pia kuongeza thamani kwa wanahisa.
Mkutano Mkuu wa Mwaka umeidhinisha gawio la mwisho la TZS 23.91 kwa kila hisa ya kawaida kwa mwaka wa fedha 2026.
Gawio hilo litalipwa ifikapo au kabla ya Oktoba 15, 2026, kwa wanahisa waliokuwa kwenye orodha ya wanahisa kufikia mwisho wa biashara tarehe Agosti 19, 2026.
Kwa ujumla, gawio linalopendekezwa kwa mwaka wa fedha 2026 linafikia TZS 53.6 bilioni, sawa na ongezeko la 18.4%ikilinganishwa na mwaka uliopita.
Ongezeko hilo linaakisi sera ya Kampuni ya kutoa thamani endelevu kwa wanahisa huku ikiendelea kuelekeza mtaji katika uwekezaji wa muda mrefu na ukuaji wa biashara.
VODACOM YACHANGIA TZS 848 BILIONI SERIKALINI
Mbali na thamani inayotokana moja kwa moja kwa wanahisa, Vodacom Tanzania imeendelea kuwa na mchango mkubwa katika uchumi wa Tanzania.
Katika mwaka wa fedha 2026, Kampuni ilichangia TZS 848 bilioni katika mapato ya Serikali kupitia kodi, tozo, ada za masafa ya mawasiliano na ada za udhibiti.
Aidha, Kampuni ilitumia TZS 839 bilioni kwa wazabuni na washirika wa ndani wapatao 400, huku ikiwekeza TZS 6.9 bilioni katika mipango mbalimbali ya kijamii.
Vodacom pia imewezesha ajira zisizo za moja kwa moja kwa zaidi ya Watanzania 320,000, wakiwemo wafanyakazi huru na mawakala wa M-Pesa.
USIMAMIZI MAKINI WA FEDHA
Akizungumzia matokeo hayo, Mkurugenzi wa Fedha wa Vodacom Tanzania Plc, Hilda Bujiku, alisema matokeo ya mwaka wa fedha 2026 yanaonyesha usimamizi makini wa fedha pamoja na mtazamo wenye uwiano katika matumizi ya mtaji.
Alisema Kampuni imeendelea kuimarisha biashara huku ikiwekeza kwa kiasi kikubwa katika mtandao, teknolojia na majukwaa ya kidijitali, hatua ambayo imewezesha kuongeza thamani kwa wanahisa.
Kwa mujibu wa Bujiku, mwelekeo huo unaiweka Vodacom Tanzania katika nafasi nzuri ya kuendeleza ukuaji, kudumisha uimara wa kifedha na kutumia fursa zinazotokana na ukuaji wa uchumi wa kidijitali nchini.
MWELEKEO WA VODACOM KUELEKEA SOKO LA KIDIJITALI
Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa Vodacom Tanzania Plc, Philip Besiimire, alisema matokeo hayo yanaonyesha umuhimu wa kuwa na mtazamo wa muda mrefu katika uwekezaji na ukuaji wa biashara.
Alisema imani ya wanahisa imeiwezesha Kampuni kuendelea kuwekeza katika mtandao, teknolojia na huduma za kifedha za kidijitali, huku ikiendelea kuboresha utendaji wa biashara na kutoa thamani endelevu kwa wanahisa.
Besiimire aliongeza kuwa Kampuni itaendelea kujenga biashara imara, yenye uwezo wa kuhimili changamoto na iliyo tayari kunufaika na fursa za siku zijazo.
UTABORA BORA NA UWEKEZAJI WENYE NIDHAMU
Mwenyekiti wa Bodi ya Vodacom Tanzania Plc, David Tarimo, alisema imani na uungwaji mkono unaoendelea kutolewa na wanahisa ni msingi muhimu wa uwezo wa Kampuni kujenga thamani endelevu kwa muda mrefu.
Alisema Vodacom itaendelea kuzingatia uwekezaji wenye nidhamu, utawala bora na usimamizi wenye uwajibikaji wa mitaji ya wanahisa.
Kwa mujibu wa Tarimo, mafanikio yaliyopatikana katika mwaka wa fedha 2026 yanaweka msingi imara wa ukuaji unaoendelea na kuongeza mchango wa Kampuni katika uchumi wa kidijitali nchini Tanzania.
VODACOM KUENDELEA KUWEKEZA KATIKA UCHUMI WA KIDIJITALI
Katika kipindi kijacho, Vodacom Tanzania inatarajia kuendelea kuwekeza katika miundombinu ya mtandao, huduma za kifedha za kidijitali, teknolojia, ubunifu na kuboresha uzoefu wa wateja.
Kampuni pia itaendelea kuimarisha ushirikiano na wadau mbalimbali wenye lengo la kuchochea maendeleo ya kidijitali na kiuchumi nchini Tanzania.
Vodacom Tanzania imeeleza kuwa itaendelea kuelekeza uwekezaji wake katika matokeo ya muda mrefu, kuimarisha utendaji wa biashara, kuboresha huduma kwa wateja, kuongeza thamani kwa wanahisa na kuleta mchango chanya kwa jamii.
Endelea kufuatilia Kitomari Banking & Finance Blog kwa habari, uchambuzi na taarifa za hivi karibuni kuhusu sekta ya benki, fedha, biashara na uchumi Tanzania.

.jpeg)
.jpeg)

No comments:
Post a Comment