![]() |
Baadhi ya wajumbe wa kamati ya maandalizi ya mbio za NBC Dodoma Marathon wakifutilia mkutano huo. |
Dodoma, 26 Julai 2024: Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Bi Rosemary Senyamule amethibitisha kukamilika kwa maadalizi ya msimu wa tano mbio za NBC Dodoma Marathon huku akionyesha kuridhishwa na ubora wa mbio hizo sambamba na mchango wake katika kuchochea kasi ya Uchumi wa mkoa huo kupitia sekta za biashara, michezo na utalii.
Mbio zinatarajiwa kufanyika Julai 28 mwaka huu kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma zikiwa na lengo la kukusanya fedha ili kusaidia mapambano dhidi ya saratani ya shingo ya kizazi na kutoa ufadhili wa elimu kwa wakunga ili kuboresha afya ya mama na mtoto. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa anatarajiwa kuongoza washiriki zaidi ya 8,000 waliothibitisha kushiriki mbio hizo.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma leo RC Senyamule pamoja na kuipongeza benki hiyo kwa maandalizi hayo mazuri alisema ujio wa mbio hizo mkoani humo kwa miaka mitano sasa umekuwa ukiambatana na fursa mbalimbali ikiwemo ongezeko la mzuguko wa fedha unaotokana na ongezeko la mahitaji ya chakula, vinywaji,mavazi na malazi kutona na idadi kubwa ya watu wanaotoka mikoa mbalimbali ili kushiriki mbio hizo jijini humo.
“Kukamilika kwa maadalizi ya mbio hizo tena katika viwango vya kimataifa kunatoa taswira sahihi ya hadhi ya mbio hizo na jiji la Dodoma kama makao makuu ya nchi. Nitoe wito kwa wananchi wa jiji la Dodoma hususani wafanyabiashara kuchangamkia fursa mbalimbali zitokanazo na ongezeko hili la watu ambao nje ya washiriki hao 8,000 waliothibitisha kushiriki pia wapo wengine zaidi walioambatana nao.’’ Alisema.