Rungwe/Kyela, Mbeya — Mei 20, 2026 — Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) imezindua rasmi kampeni yake ya “Wekeza NBC Shambani Ushinde” katika wilaya za Rungwe na Kyela mkoani Mbeya, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa benki hiyo wa kuimarisha ujumuishaji wa huduma za kifedha kwa wakulima na kuchochea maendeleo ya sekta ya kilimo nchini.
Uzinduzi huo umepokelewa kwa pongezi kutoka kwa viongozi wa Serikali katika wilaya hizo, huku Wakuu wa Wilaya ya Rungwe na Kyela, Bw. Jaffar Haniu na Bi. Josephine Manase, wakieleza kuvutiwa na namna kampeni hiyo ilivyolenga kuwainua wakulima kupitia huduma za bima, elimu ya fedha pamoja na suluhisho mbalimbali za kifedha zinazokidhi mahitaji ya sekta ya kilimo.
Kupitia kampeni hiyo, NBC inalenga kuongeza tija na uzalishaji wa mazao ya kimkakati yakiwemo kahawa, kakao na ufuta kwa kuwafikia wakulima mmoja mmoja, AMCOS pamoja na vyama vikuu vya ushirika kupitia huduma maalum za kibenki, elimu ya kifedha na bidhaa bunifu zinazosaidia kukuza kilimo-biashara.
Serikali Yapokea Kwa Pongezi Kampeni ya NBC Shambani
Uzinduzi wa kampeni hiyo ulifanyika hivi karibuni ambapo wilayani Rungwe hafla hiyo iliongozwa na Mkuu wa Wilaya, Bw. Jaffar Haniu, huku uzinduzi wa Kyela ukiongozwa na Mkuu wa Wilaya hiyo, Bi. Josephine Manase. Hafla hizo zilihudhuriwa na viongozi wa vyama vya ushirika, wakulima, wadau wa sekta ya kilimo pamoja na viongozi waandamizi wa NBC wakiongozwa na Mkurugenzi wa Idara ya Wateja Binafsi na Biashara Ndogo wa benki hiyo, Bw. Elibariki Masuke.
Akizungumza katika uzinduzi wa kampeni hiyo wilayani Rungwe, Bw. Haniu aliipongeza NBC kwa kuendelea kubuni huduma za kifedha zinazowalenga moja kwa moja wakulima na kusaidia kuchochea ukuaji wa uchumi katika maeneo ya vijijini.
Alisema huduma za bima zinazotolewa kupitia kampeni hiyo, ikiwemo bima ya mazao, mifugo, misitu na afya, zina mchango mkubwa katika kupunguza athari za kiuchumi zinazotokana na majanga mbalimbali pamoja na kuwahakikishia wakulima usalama wa shughuli zao za uzalishaji.
“Mbali na motisha ya zawadi mbalimbali zinazotolewa kupitia kampeni hii, jambo kubwa zaidi ni namna NBC ilivyogusa mahitaji halisi ya wakulima kupitia elimu ya fedha, mikopo ya kilimo na huduma za bima ambazo zitawawezesha wakulima kuongeza tija na kupanga vizuri matumizi ya mapato yao,” alisema Bw. Haniu.






.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)








.jpeg)
.jpeg)













.jpeg)



.jpeg)
