Dar es Salaam, Mei 12, 2026 — Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) imezindua kampeni mpya ijulikanayo kama “Shinda Trip ya Mauritius”, yenye lengo la kuhamasisha matumizi ya mifumo ya malipo ya kidijitali kupitia kadi za NBC Visa huku ikiwapa wateja nafasi ya kujishindia safari ya kifahari kwenda visiwa vya Mauritius.
Kampeni hiyo ya miezi mitatu ilizinduliwa rasmi katika makao makuu ya benki hiyo jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na viongozi wa benki, wafanyakazi, waandishi wa habari pamoja na wadau mbalimbali wa sekta ya huduma za kifedha.
NBC Yaongeza Kasi ya Uchumi Usio wa Fedha Taslimu
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkuu wa Idara ya Masoko wa NBC, David Raymond alisema kampeni hiyo inalenga kuwahamasisha wateja kutumia zaidi mifumo ya malipo ya kidijitali kwa kufanya manunuzi na miamala mbalimbali kupitia kadi za NBC Visa ndani na nje ya Tanzania.
Alieleza kuwa mpango huo ni sehemu ya dhamira pana ya NBC katika kuendeleza uchumi usiotegemea fedha taslimu pamoja na kuimarisha ujumuishaji wa kifedha kupitia huduma za kisasa, salama na rahisi kutumia.
“Tunalenga kuona wateja wetu wanakumbatia kikamilifu matumizi ya malipo ya kidijitali kwa sababu ni salama zaidi, yanafanyika kwa haraka na ni rahisi zaidi katika maisha ya sasa. Dunia inaelekea katika matumizi ya mifumo janja ya kifedha, na sisi NBC tunataka kuhakikisha wateja wetu wanakuwa sehemu ya safari hiyo,” alisema Raymond.
Namna ya Kushiriki Kampeni
Kupitia kampeni hiyo, kila mteja atakayefanya miamala mitano au zaidi kwa kutumia kadi ya NBC Visa ataingia moja kwa moja kwenye droo ya kila mwezi.
Washindi watakaobahatika watajishindia safari ya gharama zote kulipiwa kwenda Mauritius. Jumla ya washindi watatu wanatarajiwa kupatikana katika kipindi chote cha kampeni, huku kila mshindi akipata nafasi ya kusafiri akiwa ameambatana na mtu mmoja wa chaguo lake.





.jpeg)









.jpeg)



.jpeg)



.jpeg)








.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)

