DODOMA, Julai 22, 2026: Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb.), anatarajiwa kuongoza zaidi ya washiriki 13,000 katika msimu wa saba wa NBC Dodoma Marathon, utakaofanyika Julai 26, 2026 katika Uwanja wa Jamhuri, jijini Dodoma.
Wakati maandalizi ya mbio hizo yakifikia tamati, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Bi. Rosemary Senyamule, ametoa wito kwa madereva kutumia Barabara ya Mzunguko (Ring Road) siku ya mbio hizo ili kupunguza msongamano wa magari katikati ya jiji na kuhakikisha usalama wa washiriki pamoja na watumiaji wengine wa barabara.
Akizungumza wakati akipokea jezi rasmi ya NBC Dodoma Marathon kutoka kwa waandaaji, Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), Bi. Senyamule alisema maandalizi ya mbio hizo yamekamilika kwa mafanikio na sasa Dodoma ipo tayari kupokea maelfu ya washiriki na wageni kutoka sehemu mbalimbali nchini.
RC Dodoma Awataka Wananchi Kushiriki na Kutoa Ushirikiano
Bi. Senyamule aliwataka wakazi wa Dodoma kujitokeza kwa wingi kandokando ya barabara kuwapa hamasa washiriki wa mbio hizo, huku akiwashauri wananchi ambao hawana ulazima wa kutumia magari yao siku hiyo kujiepusha kuyaingiza katikati ya jiji.
Aidha, aliwasihi wasafiri wanaotoka mikoa mbalimbali kutumia Ring Road ili kurahisisha mtiririko wa magari na kuhakikisha mbio zinafanyika kwa utulivu na usalama.
"Tunawaomba wananchi wajitokeze kwa wingi kuwashangilia washiriki wa mbio hizi. Kwa wale ambao hawana ulazima wa kutumia magari yao siku hiyo, ni vyema wakaepuka kuyaingiza katikati ya jiji ili kupunguza msongamano na kuhakikisha usalama wa washiriki pamoja na watumiaji wengine wa barabara," alisema.
Hafla ya kukabidhi jezi hiyo ilifanyika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali, akiwemo Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa, Bi. Mwajabu Nyamkumora, viongozi wa NBC wakiongozwa na Mkuu wa Idara ya Mawasiliano na Mahusiano ya Umma, Bw. Godwin Semunyu, pamoja na wawakilishi wa wadhamini wa mbio hizo kutoka GSM Group na Vodacom Tanzania.
Mbio za Viwango vya Kimataifa Zenye Zawadi Kubwa
Bi. Senyamule aliipongeza NBC Bank na wadau wake kwa kuandaa mbio hizo kwa viwango vya kimataifa, akisema zimeendelea kuiweka Dodoma kwenye ramani ya matukio makubwa ya michezo nchini sambamba na kuimarisha hadhi yake kama Makao Makuu ya Tanzania.
Mbio za mwaka huu zitahusisha umbali wa kilomita 5, 10, 21 na 42, huku washindi wa kwanza wa mbio za kilomita 42 kwa upande wa wanaume na wanawake kila mmoja akitarajiwa kujishindia Shilingi milioni 11.5, pamoja na bonasi ya Shilingi milioni 5 iwapo atavunja rekodi ya mwaka uliopita.
Mbio Zinazoleta Mabadiliko Kwenye Sekta ya Afya
Mbali na ushindani wa michezo, Bi. Senyamule alisema NBC Dodoma Marathon imeendelea kuwa chombo muhimu cha kuunga mkono huduma za afya kupitia ajenda zake kuu tatu ambazo ni:
- Kuchangisha fedha za kupunguza vifo vya kina mama na watoto wakati wa kujifungua.
- Kufadhili upasuaji wa watoto wenye matatizo ya moyo.
- Kuimarisha mfuko wa huduma za upandikizaji wa uloto kwa watoto wenye ugonjwa wa selimundu (Sickle Cell).
















.jpeg)
.jpeg)










.jpeg)
.jpeg)



.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)