TZS Bilioni 1 Zakusanywa Kuimarisha Afya ya Mama na Mtoto
Dodoma, Julai 26, 2026 – Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, ameongoza zaidi ya washiriki 13,000 katika NBC Dodoma Marathon 2026, huku akiipongeza Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) kwa kufanikisha ukusanyaji wa TZS bilioni 1 zitakazotumika kuboresha huduma za afya ya mama na mtoto pamoja na kuokoa maisha ya maelfu ya Watanzania.
Fedha hizo zitaelekezwa katika maeneo matatu muhimu ya kijamii ambayo ni kupunguza vifo vya akina mama na watoto wakati wa kujifungua, kugharamia upasuaji wa watoto wenye matatizo ya moyo, na kuimarisha huduma za upandikizaji wa uloto kwa watoto wanaoishi na ugonjwa wa selimundu (Sickle Cell).
NBC Dodoma Marathon Yazidi Kukua kwa Kasi
Mbio hizo, zilizofanyika katika Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma, zimeendelea kujijengea heshima kama moja ya matukio makubwa ya michezo nchini, zikivutia washiriki kutoka Tanzania na mataifa mbalimbali.
Mashindano hayo yalishuhudia ushindani mkali kati ya wanariadha wa Tanzania na Kenya katika mbio za kilomita 21 na 42, huku Dkt. Nchemba, viongozi wa Serikali, taasisi mbalimbali na sekta binafsi wakishiriki mbio za kilomita tano (5) kama sehemu ya kuhamasisha mazoezi na maisha yenye afya.
Serikali Yapongeza Ushirikiano wa Sekta Binafsi
Akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi zawadi kwa washindi na wadau wa mbio hizo, Dkt. Nchemba alisema mafanikio ya NBC Dodoma Marathon yanaonyesha nguvu ya ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi katika kuleta maendeleo yenye manufaa kwa jamii.
Alibainisha kuwa ongezeko la washiriki kutoka 1,500 mwaka 2020 hadi zaidi ya 13,000 mwaka 2026 linaonesha mwamko mkubwa wa Watanzania kushiriki michezo, kuimarisha afya zao na kuunga mkono shughuli za maendeleo kupitia michezo.
"NBC Dodoma Marathon imekuwa zaidi ya mashindano ya riadha. Leo ni jukwaa linalounganisha Watanzania na marafiki kutoka mataifa mbalimbali kwa lengo la kufanya jambo kubwa zaidi—kuokoa maisha. Nawahimiza Watanzania kujenga utamaduni wa kufanya mazoezi mara kwa mara ili kujikinga dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza kama vile kisukari, shinikizo la damu, magonjwa ya moyo na figo," alisema Dkt. Nchemba.
Aidha, alisema Serikali itaendelea kuboresha miundombinu ya barabara katika Jiji la Dodoma kwa kupanua na kuboresha barabara muhimu ili kurahisisha usafiri na kuongeza usalama wa washiriki wa mbio hizo katika miaka ijayo.







.jpeg)

.png)








.jpeg)
.jpeg)









