Uzinduzi huo umefanyika siku ya Ijumaa Aprili 25, 2025, Makao Makuu ya TCB yaliyopo eneo la Makumbusho, jijini Dar es Salaam, ukihudhuriwa na wadau mbalimbali wa benki, wafanyakazi, wateja, pamoja na wawakilishi wa vyombo vya habari.
Akizungumza kwa niaba ya Afisa Mtendaji Mkuu wa TCB, Adam Mihayo, Mkurugenzi wa Wateja Binafsi na Wafanyabiashara Wadogo na wa Kati, Bi. Lilian Mtali, amesema kuwa benki hiyo imeamua kuwekeza zaidi ya shilingi milioni 200 katika kampeni hii kama sehemu ya kurudisha kwa jamii, lakini pia kama njia ya kuendelea kukuza matumizi ya teknolojia ya kifedha nchini.
“Hii ni namna ya kuwarudishia wateja wetu, jamii na wafanyabiashara wadogo wanaotuzunguka. Tumepanga kuwazawadia washindi mbalimbali watakaoibuka kidedea kupitia miamala wanayofanya kwa njia ya kidijiti kwa kipindi cha miezi minne,” amesema Mtali.
Ameongeza kuwa TCB imekuwa mstari wa mbele katika kuwekeza kwenye ubunifu wa mifumo ya huduma za kifedha ili kumwezesha Mtanzania kufanya miamala kwa haraka, kwa usalama na mahali popote, bila kulazimika kufika tawi la benki.
“Kwa kutumia huduma kama Popote Mobile App, Popote Visa Card, na mfumo wa Lipa Popote, mteja anaweza kufanya miamala bila usumbufu. Tunasisitiza uhuru wa kujihudumia kibenki kwa kutumia teknolojia kwa sababu muda ni pesa,” amesema Mtali.
Kwa upande wake, Jesse Jackson, Afisa Mkuu wa Huduma za Kidijiti na Ubunifu wa TCB, amesema kuwa kupitia kampeni ya Toboa Kidijitali, benki hiyo inatarajia kutoa zawadi mbalimbali kwa washindi, ikiwemo gari aina ya Mazda, simu ya iPhone 16 Pro Max, bajaji, bodaboda kila mwezi kwa kipindi cha miezi minne.
Jackson amesema kuwa kampeni hii inalenga si tu kuongeza miamala ya kidijitali, bali pia kuchochea ujumuishi wa kifedha kwa makundi yote ya Watanzania, wakiwemo wale wa vijijini na maeneo ya pembezoni.



















































