Blog Rebranding Teaser_030826

Blog Rebranding Teaser_030826

Stanbic Bank Banner_070826

Stanbic Bank Banner_070826

Absa Loan Campaign_160426

Absa Loan Campaign_160426

Monday, 14 September 2026

TBL NA VODACOM TANZANIA WAINGIA MAKUBALIANO YA KUWAWEZESHA WAFANYABIASHARA ZAIDI YA 26,000

Mkurugenzi wa Vodacom Business, Nguvu Kamando (kushoto), akimkabidhi zawadi ya ukumbusho Mkurugenzi Mtendaji wa Tanzania Breweries Limited (TBL), Bi. Michelle Kilpin (kulia), mara baada ya hafla ya kusaini Makubaliano ya Ushirikiano (MoU) kati ya kampuni hizo mbili, iliyofanyika jijini Dar es Salaam, Septemba 11, 2026. Kupitia ushirikiano huo, zaidi ya wafanyabiashara 26,000 wa TBL nchini watanufaika na mafunzo ya biashara pamoja na suluhisho za kidijitali za Vodacom kupitia Mpango wa Maendeleo ya Wafanyabiashara wa Rejareja (Retailer Development Programme).

Ushirikiano wa kimkakati kuwawezesha wafanyabiashara kupata ujuzi, teknolojia na suluhisho za kidijitali

• Mpango huo wazinduliwa rasmi Mwanza Septemba 16

Dar es Salaam, Septemba 11, 2026: Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) na Vodacom Tanzania PLC zimeingia makubaliano ya ushirikiano (MoU) ya miaka miwili, yenye lengo la kuimarisha uwezo wa wafanyabiashara nchini kupitia Mpango wa Maendeleo ya Wafanyabiashara wa Rejareja (Retailer Development Programme).

Mpango huo umebuniwa kuwawezesha wafanyabiashara kupata ujuzi wa vitendo katika usimamizi wa biashara, fedha na matumizi ya teknolojia, kwa lengo la kukuza biashara zao na kuongeza mchango wao katika ukuaji wa uchumi.

Ukiendeshwa chini ya kaulimbiu “Growing Innovatively Together” (GRIT), mpango huo unaonesha dhamira ya pamoja ya TBL na Vodacom Tanzania kuwawezesha wafanyabiashara wanaoshiriki katika mnyororo wa thamani wa TBL, huku wakiimarisha mchango wao katika uchumi wa Tanzania.

TBL: Wafanyabiashara ni Nguzo Muhimu

Akizungumza wakati wa hafla ya kusaini makubaliano hayo, Mkurugenzi wa Masuala ya Kisheria na Uhusiano wa Kampuni wa TBL, Neema Temba, alisema ushirikiano huo unaonesha umuhimu wa kuwekeza katika uwezo wa wafanyabiashara ili kuwawezesha kukua kwa muda mrefu.

“Kwa TBL, wafanyabiashara ni nguzo muhimu ya biashara na ukuaji wa uchumi. Kupitia ushirikiano na Vodacom Tanzania, tunawekeza katika ujuzi, teknolojia na uendelevu wa biashara ili kuwawezesha kukuza shughuli zao na kunufaika na fursa mpya. Hivyo tunajenga thamani inayonufaisha biashara, familia na jamii kote nchini,” alisema Bi. Temba.

 

Ushirikiano huo utaunganisha mtandao wa TBL wa zaidi ya wafanyabiashara 26,000 na uzoefu wa Vodacom Tanzania katika mawasiliano, ubunifu wa kidijitali na huduma za kifedha, kwa lengo la kuwasaidia wafanyabiashara kuboresha ufanisi, uimara na uendelevu wa biashara zao.

Mafunzo katika Maeneo Muhimu ya Biashara

Kupitia mpango huo, wafanyabiashara watapatiwa mafunzo katika maeneo mbalimbali muhimu ya uendeshaji wa biashara, yakiwemo usimamizi wa biashara na fedha, mtiririko wa fedha, usimamizi wa bidhaa, mauzo na masoko, huduma kwa wateja, ujasiriamali, biashara inayozingatia uwajibikaji pamoja na matumizi ya teknolojia za kidijitali.

Mbali na mafunzo, washiriki watawezeshwa kupata uelewa na kutumia suluhisho za kidijitali na kifedha zinazoweza kuwasaidia kuongeza ufanisi wa biashara, kuboresha faida na kuimarisha mahusiano na wateja.

Vodacom: Teknolojia kwa Ukuaji wa Biashara

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Vodacom Business, Nguvu Kamando, alisema ushirikiano huo ni sehemu ya dhamira ya Vodacom Tanzania ya kutumia teknolojia na ubunifu kusaidia wafanyabiashara na kuchochea ukuaji wa biashara nchini.

“Biashara ndogo ni muhimili wa uchumi wa Tanzania. Kupitia ushirikiano wa TBL na Vodacom Tanzania, wafanyabiashara wanapatiwa zana, maarifa na teknolojia za kuboresha biashara, kuongeza tija na kufungua fursa za ukuaji endelevu. Kwa pamoja, tunachochea ujumuishaji wa kidijitali na kifedha, na kuwawezesha kustawi katika uchumi unaoongozwa na teknolojia,” alisema Bw. Kamando.

Katika utekelezaji wa mpango huo, Vodacom itawapatia wafanyabiashara fursa ya kufahamu na kutumia suluhisho mbalimbali za biashara na huduma za kidijitali, ikiwemo SME Bomba, M-Wekeza, Lipa kwa M-Pesa na M-Koba.

Suluhisho hizo zinalenga kusaidia ujumuishaji wa huduma za kifedha, kuongeza ufanisi wa biashara na kuwezesha matumizi ya teknolojia katika shughuli za kila siku.

Mafunzo ya Kwanza Kufanyika Mwanza

Kadhalika, ushirikiano huo utakuza ubunifu, ujasiriamali na uwajibikaji katika biashara kupitia mafunzo ya ana kwa ana pamoja na majukwaa ya kidijitali.

TBL na Vodacom Tanzania pia zitashirikiana katika mawasiliano, ushirikishwaji wa wadau, ufuatiliaji na tathmini ya mpango huo ili kuhakikisha unazalisha matokeo yanayopimika na yenye manufaa ya muda mrefu.

Mafunzo ya kwanza chini ya Mpango wa Maendeleo ya Wafanyabiashara wa Rejareja yatafanyika jijini Mwanza, Septemba 16, 2026, yakiwa na lengo la kuwapatia wafanyabiashara ujuzi wa usimamizi wa biashara, fedha na matumizi ya teknolojia kwa ajili ya kuboresha utendaji na kukuza biashara zao kwa uendelevu.

Kupitia ushirikiano huu, TBL na Vodacom Tanzania zinaendelea kuimarisha ujasiriamali, matumizi ya huduma za kidijitali na ujumuishaji wa kifedha, huku zikiwawezesha wafanyabiashara kuchangia zaidi katika ukuaji wa uchumi wa Tanzania.


📌 Endelea Kufuatilia Kitomari Banking & Finance Blog

Kwa habari zaidi, uchambuzi na taarifa za kina kuhusu benki, fedha, biashara, uwekezaji na uchumi, endelea kutembelea Kitomari Banking & Finance Blog.

Tufuatilie kwenye mitandao yetu ya kijamii:

LinkedIn | Facebook | Instagram | X (Twitter)

No comments:

Post a Comment