Blog Rebranding Teaser_030826

Blog Rebranding Teaser_030826

Stanbic Bank Banner_070826

Stanbic Bank Banner_070826

Absa Loan Campaign_160426

Absa Loan Campaign_160426

Thursday, 20 August 2026

VODACOM TANZANIA YAUNGA MKONO ELIMU JUMUISHI, YABORESHA MAZINGIRA YA KUJIFUNZIA KATIKA SHULE TATU

Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya ya Mkuranga, Helen Kulwa Benjamini (kushoto), akishikana mkono na Meneja Mauzo Mwandamizi wa Kanda ya Dar es Salaam na Pwani wa Kampuni ya Vodacom Tanzania Plc, George Nyanda (kulia), wakati wa makabidhiano ya madarasa mawili yaliyoboreshwa pamoja na madawati 30 katika Shule ya Msingi Vikindu, chini ya mpango wa kampuni hiyo wa kurejesha kwa jamii. Msaada huo umetolewa kwa lengo la kuwawezesha wanafunzi kupata mazingira bora ya kujifunzia. Hafla hiyo ilifanyika tarehe 14 Agosti 2026 huko Vikindu, Mkoa wa Pwani.
Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya ya Mkuranga, Madam Helen Kulwa Benjamini (kulia), akishikana mkono na Meneja Mauzo Mwandamizi wa Kanda ya Dar es Salaam na Pwani wa Kampuni ya Vodacom Tanzania Plc, George Nyanda (kushoto), wakati wa makabidhiano ya madarasa mawili yaliyorekebishwa pamoja na madawati 30 yaliyotolewa na kampuni hiyo. Tukio hilo lilishuhudiwa na Mwenyekiti wa Kijiji cha Vikindu, Said Nguvumari (kulia), pamoja na Mwenyekiti wa CCM Kata ya Vikindu, Bahati Ali Mawinga.

Dar es Salaam, Tanzania – 14 Agosti 2026

Vodacom Tanzania, kupitia Vodacom Tanzania Foundation, inaendelea kuchangia katika kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa watoto nchini kupitia ukarabati na ujenzi wa madarasa katika shule tatu za msingi za umma zilizopo mikoa ya Pwani, Ruvuma na Morogoro.

Mpango huo unaotekelezwa kwa kuzingatia mahitaji yaliyobainika katika jamii, unalenga kuimarisha mazingira ya elimu, hususan kwa watoto wenye mahitaji maalum katika shule za umma.

Kupitia mpango huo, jumla ya madarasa sita yameboreshwa katika Shule za Msingi Vikindu wilayani Mkuranga, Pwani; Mahilo mkoani Ruvuma; na Ihowanja mkoani Morogoro, ambapo kila shule imepatiwa madarasa mawili. Kati ya madarasa hayo, mawili yamekarabatiwa huku manne yakijengwa upya.

Maboresho hayo yanatarajiwa kunufaisha jumla ya wanafunzi 4,838, wakiwemo 117 wenye mahitaji maalum, pamoja na walimu 52. Aidha, Vodacom Tanzania imetoa jumla ya madawati 90 kwa shule hizo tatu.

VODACOM YAKABIDHI MADARASA VIKINDU

Hafla ya kwanza ya makabidhiano ilifanyika katika Shule ya Msingi Vikindu, Wilaya ya Mkuranga, ambapo Vodacom Tanzania ilikabidhi madarasa yaliyoboreshwa pamoja na madawati kwa uongozi wa shule.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, George Nyanda, Meneja Mauzo Kanda ya Dar es Salaam na Pwani wa Vodacom Tanzania, alisema uwekezaji huo unalenga kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa wanafunzi na kufundishia kwa walimu.

“Katika Shule ya Msingi Vikindu, madarasa haya mawili yanalenga kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa watoto na kufundishia kwa walimu. Kuitikia mahitaji ya jamii kunahitaji kuelewa mambo yanayoweza kuleta tofauti katika maisha ya kila siku ya watoto, hususan wale wenye mahitaji maalum,” alisema Nyanda.

Aliongeza kuwa Vodacom Tanzania inafurahia kuchangia katika kujenga mazingira yatakayowawezesha wanafunzi kujifunza kwa utulivu na kujisikia kuwa sehemu ya jamii ya shule.

MADARASA MAPYA KUONGEZA FURSA ZA ELIMU IHOWANJA

Katika Shule ya Msingi Ihowanja, Morogoro, Chiha Nchimbi, Mkuu wa Kanda ya Kati wa Vodacom Tanzania, alisema madarasa mawili mapya yataongeza nafasi muhimu za kujifunzia kwa wanafunzi.

“Katika Shule ya Msingi Ihowanja, madarasa haya mawili mapya yanaongeza nafasi muhimu za kujifunzia kwa jamii ya shule. Haya ni maeneo ambayo yatatumika kila siku kwa ajili ya masomo, kukuza ujuzi na kuwawezesha watoto kuendelea kujifunza na kukua,” alisema Nchimbi.

Kwa mujibu wa Nchimbi, uwekezaji huo unaakisi dhamira ya Vodacom Tanzania Foundation ya kuitikia mahitaji halisi ya jamii kupitia mipango yenye matokeo ya moja kwa moja.

MAHILO KUPATA MADARASA MAPYA

Akizungumzia manufaa ya mradi huo katika Shule ya Msingi Mahilo mkoani Ruvuma, Abednego Mhagama, Mkuu wa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini wa Vodacom Tanzania, alisema madarasa hayo mawili mapya yatawapatia wanafunzi na walimu mazingira bora zaidi ya kujifunzia na kufundishia.

“Darasa si jengo pekee; ni sehemu ambayo watoto hutumia muda wao mwingi kujifunza na kujiandaa kwa maisha yao ya baadaye. Tunafurahi kuchangia katika kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa jamii hii,” alisema Mhagama.

Hafla ya makabidhiano katika Shule ya Msingi Mahilo mkoani Ruvuma inatarajiwa kufanyika tarehe 20 Agosti 2026, huku makabidhiano katika Shule ya Msingi Ihowanja, Morogoro yakipangwa kufanyika tarehe 27 Agosti 2026.

VODACOM TANZANIA FOUNDATION YAENDELEA KUWEKEZA KATIKA ELIMU

Maboresho ya madarasa katika shule hizo tatu ni sehemu ya mchango unaoendelea wa Vodacom Tanzania Foundation katika kusaidia sekta ya elimu na kuboresha mazingira ya kujifunzia katika jamii mbalimbali nchini.

Kupitia programu zake za kijamii, Foundation imeendelea kuelekeza rasilimali katika maeneo yenye mahitaji yaliyobainika, ikilenga kusaidia kujenga mazingira ambayo yanawawezesha watoto kupata elimu katika mazingira salama, rafiki na jumuishi.

Msaada huo pia unaendana na umuhimu wa elimu jumuishi, inayolenga kuhakikisha watoto wote, wakiwemo wenye mahitaji maalum, wanapata fursa sawa za kujifunza na kushiriki kikamilifu katika mazingira ya shule.

Vodacom Tanzania Foundation inaendelea kushirikiana na jamii na wadau mbalimbali katika kutekeleza miradi inayolenga kuleta matokeo chanya na ya kudumu katika maisha ya Watanzania.

Endelea kufuatilia Kitomari Banking & Finance Blog kwa habari zaidi kuhusu benki, biashara, fedha, uwekezaji, teknolojia na maendeleo ya kijamii nchini Tanzania.

No comments:

Post a Comment