Dar es Salaam – Februari 26, 2026
Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) imekabidhi zawadi kuu za kampeni yake ya “Ukigusa Tu, iMOOO”, ikiwemo gari aina ya Nissan X-Trail kwa mshindi wa zawadi kuu, Bw. Salah Ahmed Mohamed, mkazi wa Dar es Salaam. Kampeni hiyo imelenga kukuza ujumuishaji wa kifedha kupitia uchocheaji wa matumizi ya huduma za kifedha za kidigitali.
Hafla ya makabidhiano imefanyika katika tawi la NBC Mlimani City, wilayani Ubungo, jijini Dar es Salaam. Mbali na mshindi wa zawadi kuu, washindi wa pili na wa tatu pia walikabidhiwa zawadi zao—simu janja aina ya iPhone 17 Pro pamoja na jiko la gesi na umeme. Hafla hiyo iliongozwa na Mkurugenzi wa Idara ya Wateja Binafsi (wadogo na wakubwa), Bw. Elibariki Masuke, akishirikiana na maofisa wengine wa benki hiyo.
Kampeni Yenye Dhamira ya Kijamii
Akizungumza katika hafla hiyo, Bw. Masuke alisema kuwa pamoja na kutoa zawadi, kampeni hiyo ilikuwa na dhamira pana ya kijamii ya kuongeza uelewa na matumizi ya huduma za kifedha za kidigitali kwa makundi mbalimbali ya jamii.
Alieleza kuwa walengwa wa kampeni hiyo walijumuisha wafanyakazi, wafanyabiashara wadogo na wa kati (SMEs), wanafunzi pamoja na wateja binafsi kutoka maeneo mbalimbali ya nchi. Lengo kuu lilikuwa kurahisisha upatikanaji wa huduma za kifedha na kupunguza changamoto za miamala ya ana kwa ana.
“Katika dunia ya leo, huduma za kifedha za kidigitali si anasa tena, bali ni nyenzo muhimu ya kurahisisha maisha ya kila siku. Kupitia kampeni hii, tumeshuhudia ongezeko la matumizi ya kadi, mashine za POS na programu tumizi ya NBC Kiganjani, jambo linaloashiria mwamko chanya wa jamii kuelekea uchumi wa kidigitali,” alisema Bw. Masuke.
Aliongeza kuwa mbali na washindi wakuu watatu waliokabidhiwa zawadi leo, benki hiyo imekuwa ikitoa zawadi za kila wiki kwa washindi wengine wengi, zikiwemo fedha taslimu na kompyuta mpakato, kama sehemu ya kuhamasisha tabia ya kuweka akiba, kufanya miamala salama na kutumia teknolojia kwa maendeleo binafsi na ya biashara.
Kukuza Ajenda ya Kitaifa ya Ujumuishaji wa Kifedha
Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Miamala wa NBC, Bw. Mangire Kibanda, alisema kampeni hiyo inaonesha dhamira ya benki kuunga mkono ajenda ya kitaifa ya ujumuishaji wa kifedha na ujenzi wa jamii inayotumia teknolojia kwa maendeleo.
“Benki tutaendelea kubuni programu na kampeni zenye kugusa maisha ya Watanzania, kwa kuzingatia mahitaji halisi ya jamii na mabadiliko ya teknolojia yanayoendelea duniani,” aliongeza.
Ushuhuda Kutoka kwa Washindi
Akizungumza kwa niaba ya washindi, Bi. Diana Bernard, aliyemwakilisha mshindi wa zawadi kuu, aliishukuru NBC kwa kuandaa kampeni yenye tija kwa wateja na jamii kwa ujumla. Alisema familia yao imekuwa mteja wa muda mrefu wa benki hiyo kutokana na ubora wa huduma na urahisi wa matumizi ya mifumo ya kidigitali.
“Zawadi hii si tu gari, bali ni ushuhuda wa namna taasisi za kifedha zinavyoweza kubadilisha maisha ya watu kwa kuwapa motisha ya kutumia huduma rasmi za kifedha. Huduma za kidigitali zimetusaidia kuendesha shughuli zetu binafsi na biashara kwa ufanisi mkubwa. Tunajivunia kuwa sehemu ya mabadiliko haya,” alisema.
Mbali na zawadi ya gari, mshindi wa pili Bw. Vidya Sagar alijishindia simu janja aina ya iPhone 17 Pro, huku Beatrice Chengula wa Temeke akijishindia jiko la gesi na umeme.
Mtazamo wa Kitomari Banking & Finance Blog
Kampeni ya “Ukigusa Tu, iMOOO” inaakisi mkakati mpana wa NBC wa kuimarisha matumizi ya mifumo ya kidigitali, kupunguza utegemezi wa miamala ya ana kwa ana, na kuongeza usalama na uwazi wa kifedha. Kwa kuunganisha motisha ya zawadi na elimu ya kifedha, benki inaendelea kuwa kichocheo muhimu cha mabadiliko kuelekea uchumi jumuishi na wa kidigitali nchini.
No comments:
Post a Comment