Foreign Exchange Rates

DStv Advert_090724

DStv Advert_090724

SBT Tanzania Advert_291123

Friday 20 November 2020

BENKI YA NCBA YACHANGIA HUDUMA ZA AFYA KWA WATOTO NJITI

Meneja chapa msaidizi wa Benki ya NCBA Tanzania, Nasikiwa Berya (kulia) akipata maelezo toka kwa Dkt. Deborah Maufi wa Babymoon Care ya Uholanzi namna gani ya kumuandaa mtoto aliyezaliwa njiti awe katika hali ya usalama, afya na uangalizi mzuri ili aweze kukua kwa wakati, hii ikiwa kwenye sehemu ya maadhimisho ya siku ya mtoto njiti Duniani. Hafla hiyo ilifanyika kwenye viwanja vya hospitali ya Muhimbili hivi karibuni jijini Dar es salaam.

Kama sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Watoto Njiti, Benki ya NCBA imeungana na wadau wengine kuchangia jitahada za kushugulikia tatizo hilo nchini, ikiwa pamoja na kuboresha utoaji huduma za afya kwa watoto na jamii zilizokumbwa na tatizo hilo.

Benki ya NCBA imetoa kiasi cha shilingi milioni tatu kwa Taasisi ya Dorris Mollel kama sehemu ya mchango wake kufanikisha maadhimisho ya Siku hiyo ya Kimataifa ya Watoto Njiti yaliyofanyika katika kitengo cha Afya ya Mama na Mtoto katika Hospitali ya Muhimbili juzi.

Akizungumza katika tukio hilo, Afisa Mwandamizi wa Masoko wa Benki ya NCBA, Nasikiwa Berya alisema kuwa mchango huo ni sehemu ya mikakati ya muda mrefu ya benki hiyo kuchangia huduma za afya na kuinua viwango vya maisha vya jamii yote kwa ujumla.

“Kufikia sasa benki yetu imetoa jumla ya shilingi milioni 43 katika harakati za kuwahudumia watoto njiti. Pia tumechangia ujenzi wa majengo na kutoa vifaa tiba vya kuwahudumia watoto njiti ikiwemo katika hospitaki ya wilaya ya Same,’ Nasikiwa alisema.

Pia alibainisha kuwa benki ya NCBA ina mkakati wa miaka mitatu wa kuchangia jitihada za kushugulikia changamoto za watoto njiti kwa kutoa misaada mbali mbali na kuwahamasisha wadau wengine kuchangia jithada hizo.

“Hapo awali NCBA Bank tuliandaa mashindano ya mchezo wa gofu kwa lengo la kuchangia huduma za afya kwa watoto njiti. Tuna mpango wa kuandaa mashindano matatu ya aina hiyo mwakani ambapo wadau mbali mbali watapata fursa ya kuungana nasi katika kuongeza ufanisi wa utoaji huduma kwa watoto hawa wanaozaliwa kabla ya muda,” alisema.

Takwimu za shirika la UNICEF zinaonesha kuwa kila mwaka zaidi ya watoto njiti 200,000 wanazaliwa nchini, na takriban watoto 9,500 kufariki kutokana na tatizo hilo.

No comments:

Post a Comment