MALINYI, MOROGORO - Agosti 28, 2026: Vodacom Tanzania PLC kupitia programu ya Classroom for Community Impact, iliyo chini ya Vodacom Tanzania Foundation, imekabidhi madarasa mawili yaliyokarabatiwa, madawati 30 pamoja na vifaa muhimu vya shule kwa wanafunzi wa Shule ya Msingi Ihowanja, wilayani Malinyi mkoani Morogoro.
Msaada huo ni sehemu ya juhudi za kampuni katika kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia katika shule za msingi za umma nchini, hususan kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum.
Makabidhiano hayo yaliyofanyika jana yanalenga kuchangia katika kuboresha miundombinu ya shule na kuweka mazingira salama na rafiki zaidi kwa wanafunzi na walimu.
MADARASA SITA, MADAWATI 90
Kupitia mpango huo, katika awamu hii Vodacom Tanzania imekarabati na kujenga jumla ya madarasa sita na kutoa madawati 90 katika shule tatu za msingi za umma zilizopo mikoa mbalimbali.
Shule hizo ni Vikindu wilayani Mkuranga mkoani Pwani, Ihowanja wilayani Malinyi mkoani Morogoro na Mahilowilayani Songea mkoani Ruvuma.
Katika Shule ya Msingi Ihowanja, msaada huo umehusisha ukarabati wa madarasa mawili pamoja na utoaji wa madawati 30. Aidha, wanafunzi wamepatiwa mahitaji muhimu ya shule, ikiwemo madaftari, chupa za kubebea maji, kalamu na mabegi.
VODACOM YAWEKEZA KATIKA ELIMU JUMUISHI
Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Mkuu wa Kanda ya Kati wa Vodacom Tanzania PLC, Chiha Nchimbi, alisema mpango huo ni sehemu ya mchango wa kampuni katika kusaidia jamii na kuboresha mazingira ambayo watoto wanapata elimu.
Alisema uwepo wa madarasa salama, madawati ya kutosha na mazingira rafiki ya kujifunzia ni muhimu katika kuwawezesha wanafunzi, hasa wenye mahitaji maalum, kushiriki kikamilifu katika masomo yao.
“Tunatambua kuwa mazingira bora ya kujifunzia yana nafasi muhimu katika kuwasaidia watoto kupata elimu bora. Ndiyo maana tunaendelea kushirikiana na jamii kuboresha miundombinu na mazingira ya shule,” alisema Nchimbi.
SHULE YASHUKURU VODACOM
Kwa upande wake, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Ihowanja, Iddy Mgonja, aliishukuru Vodacom Tanzania kwa msaada huo, akisema utakuwa na mchango mkubwa katika kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia shuleni hapo.
Mgonja alisema ukarabati wa madarasa mawili, kupatiwa madawati 30 pamoja na vifaa muhimu vya shule utasaidia kupunguza changamoto ya upungufu wa madarasa na madawati.
Aliongeza kuwa mazingira hayo yatawawezesha wanafunzi kusoma katika hali salama na rafiki zaidi, huku walimu wakipata mazingira bora ya kutekeleza majukumu yao ya kufundisha.
SERIKALI, JAMII WAPONDEZA MSAADA
Makabidhiano hayo yalishuhudiwa na Diwani wa Kata ya Kilosampepo, Boniventure Killian Mwanga, pamoja na Mtendaji wa Kijiji cha Ihowanja, Gotard Garus Mitti, viongozi wa jamii na wadau wengine wa elimu.
Viongozi hao wamepongeza uwekezaji huo wakisema utasaidia kupunguza changamoto za miundombinu ya elimu na kuweka mazingira bora na salama zaidi kwa wanafunzi na walimu.
Wamesisitiza kuwa ushirikiano kati ya sekta binafsi, Serikali na jamii ni muhimu katika kuharakisha upatikanaji wa miundombinu bora na jumuishi ya elimu, hususan kwa watoto wenye mahitaji maalum.
KUJENGA MAZINGIRA JUMUISHI YA ELIMU
Programu ya Classroom for Community Impact ni sehemu ya jitihada za Vodacom Tanzania kupitia Vodacom Foundation za kushirikiana na jamii katika kuboresha mazingira ya elimu na kusaidia kujenga mazingira jumuishi zaidi ya kufundishia na kujifunzia kwa watoto nchini.
Kupitia uwekezaji huo, Vodacom Tanzania inaendelea kuunga mkono juhudi za kuboresha miundombinu ya shule za umma na kuhakikisha wanafunzi wanapata mazingira yanayowawezesha kujifunza kwa usalama na ufanisi.
Endelea kufuatilia Kitomari Banking & Finance Blog kwa habari zaidi kuhusu biashara, benki, fedha, uwekezaji na maendeleo ya kijamii nchini Tanzania.

.jpeg)
.jpeg)

No comments:
Post a Comment