Foreign Exchange Rates

CRDB Bank Advert_070325

Selcom Pesa Advert_110225

Selcom Pesa Advert_110225

Standard Chartered Advert_300125

Standard Chartered Advert_300125

Wednesday, 30 July 2025

WADAU WAONYA KUHUSU ONGEZEKO LA MATUMIZI YA POMBE HARAMU NCHINI TANZANIA

Meneja wa Mradi wa Euromonitor, Benjamin Rideout, akizungumza katika mkutano wa wadau uliofanyika tarehe 30 Julai 2025 jijini Dar es Salaam, kujadili changamoto ya pombe haramu ambayo inakadiriwa kuchangia asilimia 55 ya matumizi ya pombe nchini. Mkutano huo uliandaliwa na CTI na kuhudhuriwa na wadau kutoka sekta binafsi na serikali.

Pichani kutoka kushoto: Prof. Lilian Kahale (UDSM), Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Mhe. Saad Mtambule, na Mkurugenzi Mtendaji wa Serengeti Breweries, Dkt. Obinna Anyalebechi.

DAR ES SALAAM, TANZANIA – 30 JULAI 2025 – Tanzania ni miongoni mwa nchi zenye matumizi makubwa ya pombe haramu barani Afrika, jambo ambalo linaelezwa kuwa tishio kubwa kwa afya ya umma, huku pia likiathiri mapato ya serikali na ukuaji wa sekta rasmi ya biashara ya vinywaji.

Taarifa hii imebainishwa leo jijini Dar es Salaam katika mkutano wa wadau wa sekta ya pombe, uliowakutanisha wawakilishi kutoka Serikalini, sekta binafsi na taasisi za udhibiti, kujadili njia bora za kukabiliana na changamoto hiyo. Mkutano huo ulifanyika chini ya kaulimbiu: "Kuungana Kupambana na Pombe Haramu Nchini Tanzania."

Kwa mujibu wa takwimu zilizojadiliwa katika mkutano huo, asilimia 55 ya pombe inayotumika nchini inakadiriwa kuwa haramu – ikiwemo pombe ya kienyeji isiyosajiliwa, ya magendo, na ile inayouzwa bila kulipa kodi au kukaguliwa kwa viwango vya ubora.

“Pombe haramu bado ni suala tete nchini Tanzania. Inahatarisha maisha ya watu kutokana na kutotimiza viwango vya usalama wa kiafya, huku pia ikipunguza mapato ya serikali na kushusha ushindani kwa biashara halali,” alisema Hussein Sufian, Mwenyekiti wa Shirikisho la Viwanda Tanzania (CTI).

Mkutano huo uliambatana na uzinduzi wa utafiti wa kitaifa kuhusu pombe haramu, ambao utafanyika kwa ushirikiano kati ya serikali na sekta binafsi ili kuchunguza sababu, ukubwa, na athari za biashara ya pombe isiyo halali nchini.

WAZALISHAJI WATOA MAONI

Akizungumza kwa niaba ya wazalishaji wa bia nchini, Mkurugenzi Mtendaji wa Serengeti Breweries Limited (SBL), Obinna Anyalebechi, alisema sekta ya pombe iko tayari kutumia matokeo ya utafiti huo kukuza bidhaa halali zitakazovutia watumiaji wa pombe haramu kuhamia bidhaa zilizosajiliwa.

“Tunataka kutumia ushahidi huu kubuni bidhaa bora, nafuu na salama ili kuwavuta walaji kutoka sokoni mwa pombe haramu kwenda kwenye bidhaa halali,” alisema Anyalebechi.

SERIKALI YAAHIDI KUCHUKUA HATUA ZA KISERA

Kwa upande wa Serikali, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, alieleza kuwa serikali imejipanga kutumia matokeo ya utafiti huo kuunda sera na hatua za kudhibiti pombe haramu nchini.

“Mkutano huu ni hatua muhimu katika kuratibu juhudi zetu za kupambana na biashara ya pombe haramu. Tunahitaji suluhisho la pamoja, la muda mrefu, linalotegemea takwimu na manufaa ya Watanzania,” alisema Chalamila.


KUHUSU SBL

Ilianzishwa mwaka 1988 kama Associated Breweries, Serengeti Breweries Limited (SBL) ni kampuni ya pili kwa ukubwa wa uzalishaji wa bia nchini Tanzania. Ikiwa chini ya EABL/Diageo tangu 2010, kampuni imewekeza katika viwango vya juu vya ubora wa kimataifa na imekuwa ikitoa fursa nyingi za ajira kwa Watanzania.

SBL huzalisha chapa mbalimbali za bia kama Serengeti Premium Lager, Serengeti Lite, Serengeti Lemon, Pilsner Lager, Kibo Gold, Guinness Stout, Guinness Smooth, na Senator. Pia, huchakata vileo maarufu vya kimataifa kama Johnnie Walker, Smirnoff Vodka, Baileys, na nyinginezo.


MAWASILIANO ZAIDI:

Rispa Hatibu
Meneja Mawasiliano na Uendelevu, SBL
📞 Simu: +255 685 260 901
📧 Barua pepe: Rispa.Hatibu@diageo.com


Fuatilia Blogu Yetu kwa Taarifa Zaidi

Kwa uchambuzi wa kina kuhusu masuala ya viwanda, biashara, sera, na maendeleo ya sekta binafsi nchini, endelea kufuatilia Kitomari Banking & Finance Blog – blogu yako ya kuaminika kwa habari makini za kiuchumi na kifedha.








No comments:

Post a Comment