Foreign Exchange Rates

Selcom Pesa Advert_110225

Selcom Pesa Advert_110225

Standard Chartered Advert_300125

Standard Chartered Advert_300125

DStv Advert_090724

DStv Advert_090724

Friday, 14 February 2025

TCB YAADHIMISHA MIAKA 100 KWA KUWEKEZA KATIKA UVUMBUZI WA KIDIJITALI



Benki ya Biashara Tanzania (TCB) imeadhimisha miaka 100 tangu kuanzishwa kwake kwa kuahidi kuendelea kuwekeza katika uvumbuzi wa kidijitali na kuongeza ubora wa huduma kwa wateja wake na kuwa wanayo dhamira ya kuimarisha nafasi ya TCB katika sekta ya kibenki nchini.


Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa benki hiyo, Adam Mihayo, Mkurugenzi wa Biashara za Wateja Wadogo na Kati, Lilian Mtali, aliwashukuru wafanyakazi na wateja kwa mchango wao katika mafanikio ya benki hiyo kwa karne moja.


Mafanikio haya ni matokeo ya bidii ya wafanyakazi wetu na uaminifu wa wateja wetu. Tutaendelea kuboresha mazingira ya kazi, kuimarisha huduma za kifedha, na kuwa mfano wa kuigwa katika sekta ya benki kupitia ubunifu wa kidijitali,” alisema Mtali.


Safari ya Miaka 100 ya TCB

Benki ya Biashara Tanzania (TCB) ilianzishwa mwaka 1925 wakati wa utawala wa kikoloni kwa jina la Tanganyika Post Office Savings Bank. Baada ya uhuru, benki hiyo ilibadilishwa kuwa Tanzania Postal Bank mwaka 1992, kabla ya kubadilishwa kuwa Tanzania Commercial Bank (TCB) mnamo mwaka 2021. Kupitia mageuzi hayo, benki imeendelea kukua na kuwa moja ya taasisi muhimu katika sekta ya fedha nchini Tanzania.


Kwa miaka 100, TCB imekuwa mstari wa mbele katika kutoa huduma za kifedha zinazolenga maendeleo ya wateja wa kipato cha chini, wafanyabiashara wadogo na wa kati, pamoja na taasisi kubwa. Katika miaka ya hivi karibuni, benki hiyo imeongeza kasi katika matumizi ya teknolojia za kifedha ili kuimarisha upatikanaji wa huduma za kibenki kwa Watanzania wengi zaidi.


Kampeni ya Kidijitali: Mahaba Kisiwani

Katika kuadhimisha miaka 100, TCB ilizindua kampeni ya Mahaba Kisiwani kwa lengo la kuhamasisha matumizi ya huduma za kibenki za kidijitali. Kupitia kampeni hiyo, wateja waliotumia njia za kidijitali kufanya miamala walijishindia safari ya kupumzika Zanzibar.


Ofisa Mkuu wa Huduma za Kidijitali na Ubunifu wa TCB, Jesse Jackson, alisema kuwa kampeni hiyo ni sehemu ya mkakati wa benki wa kuongeza matumizi ya mifumo ya kidijitali katika sekta ya fedha.


Kampeni ya Mahaba Kisiwani ni uthibitisho wa dhamira yetu ya kusogeza huduma za benki kwa wateja kwa njia za kisasa, salama na rahisi. Kwa kuwazawadia wateja wetu, tunawapa motisha zaidi kutumia mifumo hii ambayo inarahisisha maisha yao,” alisema Jackson.

Mmoja wa washindi wa kampeni hiyo, mfanyabiashara Maygrace Nyambuka, aliipongeza TCB kwa huduma zake bora, akieleza kuwa miamala ya kidijitali imerahisisha biashara yake na kumpunguzia gharama za kutuma na kupokea fedha.

Mustakabali wa TCB

Katika hatua inayofuata, TCB inatarajia kuendelea kuwekeza katika mifumo ya teknolojia ya kifedha, kuongeza mtandao wa matawi na wakala wa benki, na kuimarisha huduma za mikopo kwa wateja wa sekta mbalimbali.

Kwa miaka 100 ijayo, TCB inalenga kuwa benki ya kidijitali inayoongoza nchini Tanzania, ikiwa na dhamira ya kutoa huduma za kifedha zinazofikia kila Mtanzania kwa gharama nafuu na kwa ufanisi wa hali ya juu.

No comments:

Post a Comment