Foreign Exchange Rates

DStv Advert_090724

DStv Advert_090724

SBT Tanzania Advert_291123

Wednesday 21 August 2024

BENKI YA I&M YAADHIMISHA KUMBUKIZI YA MIAKA 50 KUANZISHWA KWAKE


Dar es Salaam - Agosti 19, 2024: Benki ya I&M Tanzania imesherehekea kumbukizi ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Benki hiyo nchini Kenya. Kumbukizi hiyo ilipambwa na hafla fupi iliyowaleta pamoja watu mbalimbali ikiwemo wateja wa Benki hiyo siku ya Ijumaa, Agosti 16. 


Hafla hiyo iliangazia chimbuko la benki hiyo, ilipotoka , inakoelekea na ukuaji wake wa kasi. Hafla hiyo ilifanyika katika makao makuu mapya ya Benki ya I&M Tanzania jijini Dar es Salaam na iliongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa I&M Group PLC, Bw. Sarit Raja-Shah.


Benki inajivunia pia kuzindua makao makuu yake mapya katika Barabara ya Haile Selassie, Masaki, Dar es Salaam, na kuashiria hatua muhimu katika upanuzi unaoendelea wa benki hiyo inayotoa huduma za kipekee za kibenki. Ofisi hiyo mpya, iliyo na vifaa vya kisasa imeanzishwa ili kutoa huduma za kibenki za kisasa zinazozingatia wateja. Uzinduzi huo kwa kiasi kikubwa utaongeza uwezo wa benki kuhudumia wateja wake kwa ufanisi mkubwa.


Hafla hiyo ilihudhuriwa na wageni mbalimbali, wakiwemo watu mashuhuri kutoka Taasisi za kibenki, viongozi wa makampuni, wateja na wadau mbalimbali wa benki hiyo. Maadhimisho hayo yalijumuisha hotuba zilizojaa hadithi za benki hiyo, kutoka kwa viongozi wa benki hiyo, hotuba zao zilielezea safari ya benki hiyo na michango yake katika uchumi wa Tanzania. 


Benki pia iliwapongeza wateja wake katika hafla hiyo ambapo imewatambua wateja wake wakubwa ambao wamekuwa na mchango muhimu kwa mafanikio ya benki. Tukio hilo lilikuwa kilele cha sherehe za kuadhimisha miaka 50 ya Benki hiyo ambazo zimeadhimishwa nchini Kenya, Rwanda na Uganda kwa heshima ya safari ya mafanikio ya benki hiyo tangu kuanzishwa kwake hadi kuwa mmoja wa watoa huduma wakuu wa huduma za kifedha Afrika Mashariki. 


Katika miongo mitano iliyopita, Benki ya I&M imeonyesha nia yake ya dhati ya kutoa huduma zenye ubora zinazotumia teknolojia ya kisasa na zinazochagiza maendeleo ya jamii.

Bw. Zahid Mustapha, Mkurugenzi Mtendaji wa I&M Bank TZ, alitoa shukrani zake kwa wateja, wadau, na wafanyakazi wa benki hiyo kwa usaidizi wao katika kufanikisha safari ya benki hiyo. “Maadhimisho haya ni uthibitisho wa ukuaji wa Benki katika kipindi cha miaka 50 iliyopita na hii ni ishara ya mchango wa Benki ya I&M Tanzania katika uchumi na watu wa Tanzania. 

Ofisi yetu hii mpya haiwakilishi tu ukuaji wa benki yetu lakini pia ni dhamira yetu inayoendelea ya kutoa huduma zenye ubora na ufanisi. Tunafurahia fursa zinazoletwa na ukuaji wa Taasisi za Kibenki na tunatarajia kuendelea na safari yetu ya ukuaji, iliyojaa mafanikio na inayochagiza kuongezeka kwa wadau na wateja wetu wanaothamini kazi zinazofanywa na benki yetu.” alisema Bw. Zahid.

Mwenyekiti wa Bodi ya Benki ya I&M Tanzania wakati akizungumza kwenye hafla hiyo alisema “Benki ya I&M Tanzania imejidhatiti kutoa huduma za kisasa na zenye ubora wa hali ya juu kwa wateja wetu huku ikichagiza ukuaji wa maisha ya watu katika jamii tunazohudumia katika nchi hii kubwa ya Tanzania. Kama Bodi ya Wakurugenzi, tunatoa mwongozo na uangalizi wetu wa karibu kulingana na maadili ya Taasisi yetu na kuendelea kuhamasisha utoaji wa huduma bora kwa watendaji ili kuongeza thamani ya Benki yetu hususani kwa wateja na wadau wetu. 

Hatua tulizopiga kama Benki ya I&M Tanzania zisingewezekana bila uungwaji mkono thabiti katika uidhinishaji wa udhibiti na usimamizi na Benki Kuu ya Tanzania. Kwa Benki Kuu ya Tanzania chini ya uongozi wa Mheshimiwa Bw. Emmanuel Mpawe Tutuba, tunashukuru sana”.

Kuhusu miaka 50 ya Benki yetu

Benki ya I&M imesherehekea kumbukizi yake ya Miaka 50 tangu kuanzishwa kwa kampuni hiyo mnamo mwaka 1974. Nia ya dhati ya ujasiriamali ya Mwanzilishi na Mwenyekiti Emeritus ndio iliyochagiza na kuifanya Benki ya I&M kukua kutoka shirika la kukopesha jamii hadi Taasisi inayotoa huduma za kifedha.

Taasisi hii inatoa huduma mbalimbali za kibenki na za kifedha zinazojumuisha Benki ya Biashara na Kitaasisi, Huduma za Kibenki za Kibinafsi na Biashara, Bancassurance, Usimamizi wa Mali na huduma za Ushauri zinazopatikana katika nchi 5 za Kenya, Uganda, Tanzania, Rwanda na Mauritius.

Kuhusu I&M Bank Limited

I&M Bank Tanzania Limited ni benki ya biashara nchini Tanzania yenye makao yake makuu Dar es Salaam na ni kampuni tanzu ya I&M Bank Group yenye makao yake makuu nchini Kenya. Imepewa leseni na Benki Kuu ya Tanzania, Benki Kuu na Mdhibiti wa Kitaifa wa Benki. Benki hii imedhamiria kuwa benki bora Afrika Mashariki kwa biashara za kati hadi kubwa na ina wateja lukuki. Kwa habari zaidi, tafadhali tembelea: https://www.imbankgroup.com/tz/

Kwa maswali ya waandishi wa habari, tafadhali wasiliana na:

Zainab Maalim
Mkuu wa Kitengo cha Wateja,
Zainab.Maalim@imbank.co.tz
+255765210014

No comments:

Post a Comment