Foreign Exchange Rates

DStv Advert_090724

DStv Advert_090724

SBT Tanzania Advert_291123

Wednesday 14 September 2022

NMB YAZINDUA TAWI LA 11 MKOANI TANGA


Wananchi wa Mkoa wa Tanga, hasa wanaojihusisha na kilimo, uvuvi, biashara na wajasiriamali, wametakiwa kutumia vema fursa zitokanzo na uzinduzi wa Tawi jipya la Benki ya NMB, Ngamiani, ulioenda sambamba na makabidhiano ya mabati 250 yenye thamani ya Sh. Milioni 10 kwa Shule ya Msingi Masiwani, iliyopo Ngamiani, Tanga.



Wito huo umetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Omary Mgumba, akizindua Tawi la NMB Ngamiani, ambalo ni la 11 mkoani humo, likiwa pia ni tawi la 40 katika Kanda ya Kaskazini (Tanga, Manyara, Arusha na Kilimanjaro), uliohudhuriwa na Meneja Uchumi na Takwimu wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Arusha, Ernest Ndunguru.



Akizungumza katika hafla hiyo, iliyohudhuriwa na wageni mbalimbali, wakiwemo viongozi wa Serikali na vyama vya siasa, Mgumba alisema ufunguzi wa tawi hilo la 11 mkoani mwake - kati ya matawi 40 kwenye mikoa minne ya Kanda ya Kaskazini, ni uthibitisho kwamba Tanga inakua kwa kasi kiuchumi na kibiashara.



“Serikali inatambua mchango wa sekta za fedha hasa NMB katika kutoa huduma za kibenki, tunaipongeza NMB kwa jitihada za kusogeza huduma za kibenki kwa jamii, kwani huduma hizo na sekta ya fedha kwa ujumla, ni kichocheo cha maendeleo ya mtu mmoja mmoja na taifa kwa jumla.



“Serikali imeweka mazingira mazuri sana ya kuhakikisha jamii inafikiwa na inazitumia huduma za kibenki, nashukuru NMB imekuwa ikiunga mkono juhudi za Serikali katika hili, na hivi karibuni ilitenga Sh. Bil. 200 kwa ajili ya mikopo nafuu yenye riba asilimia 9 kwenye sekta ya kilimo,” alisema Mgumba katika hafla hiyo.



Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Serikali wa NMB, Alfred Shao, alisema baada ya Sh. Bilioni 100 za kwanza ilizotenga kukopesha wadau wa kilimo kwa riba nafuu ya asilimia 10 kwisha, benki yake imeongeza kiasi hicho kwa kutenga Bil. 100 nyingine kunufaisha kada hiyo muhimu kwa ukuaji wa uchumi wa Taifa kwa asilimia 9.



Alibainisha kwamba, NMB Ngamiani linakuwa Tawi la 228 Tanzania kote, ikiwa ni miaka 25 tu tangu ilipoanzishwa (1997), ikiwa na matawi 97 tu na kwamba licha ya uwingi wa matawi hayo, mashine za kutolea fedha (ATM) 762 na Mawakala zaidi ya 15,000, lakini benki yake imejikita na kufanya mapinduzi makubwa kidijitali.

Shao alifafanua kwamba, wakulima wa mkonge na muhogo, wadau wa sekta hiyo, pamoja na wafanyabiashara, wafanyakazi na wajasiriamali mkoani Tanga, wanapaswa kuchangamkia fursa hizo ili kukua kiuchumi na kuimarisha ukuaji wa benki, hivyo kutanua faida na gawio la Serikali, na asilimia 1 ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR).

Naye Meneja Uchumi na Takwimu wa BoT, Ernest Ndunguru, aliipongeza NMB kwa kutambua na kuthamini uwepo wa BoT na kwamba mwaliko waliopewa ni uthibitisho kwamba wanathamini uwajibikaji wao, hasa ikizingatiwa kwamba wao ndio wasimamizi wakuu wa sekta ya fedha nchini.

“Uzinduzi wa NMB Tawi la Ngamiani, ni ishara kwamba NMB iko bega kwa bega na BoT katika kutekeleza sera za fedha na kuhakikisha mzunguko wa fedha na huduma za kibenki unawafikia wananchi popote kwa urahisi zaidi, uzinduzi huu pia ni ishara kwamba NMB inakubalika kwa wananchi kutokana na shughuli zake,” alisema.

No comments:

Post a Comment