Dar es Salaam: Katika kile kilichoelezwa kuwa ni kujali stori za maisha ya wajasiriamali wadogo wanaojishughulisha na uchuuzi wa maua, Benki ya Absa Tanzania imewatembelea wafanyabiashara hao, kuzungumza nao na kuwapa motisha mbalimbali, ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha Siku ya Wapendanao iliyoadhimishwa duniani kote hivi karibuni.
Akizungumza katika hafla hiyo katika eneo maarufu kwa biashara hiyo la Mbuyuni, Namanga jijini Dar es Salaam jana, Meneja wa Masuala Endelevu na Matukio wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Abigail Lukuvi, alisema Absa imeamua kuwatembelea wajasiriamali hao kama njia ya kusambaza upendo, kwa kuwa ni kati ya makundi yanayosahaulika, wakati wanahusika kwenye kusambaza upendo kwa kuuza maua.
“Hawa wafanyabiashara ndio watu muhimu sana katika kusambaza upendo, lakini mara nyingi husahaulika, hutumia siku yao nzima katika kuuza maua na kusambaza upendo kwa wengine, lakini wao wenyewe wanasahaulika, kwa hiyo Absa imeamua kuwatembelea ili wasijisikie wapweke bali wajisikie kuguswa na upendo”, alisema Bi. Abigail.
Mmoja wa wafanyabiashara hao wa maua, Robert Mwita Nyamkama, huku akiishukuru benki hiyo kwa kuwatembelea, alisema biashara ya mwaka huu imeshamiri ikilinganishwa na mwaka jana, hali inayotokana na watu wengi zaidi kuwa na mwamko wa kupeleka zawadi ya maua kwa wapendwa wao.
“Tunaishukuru Absa kwa kutukumbuka na kuja kututembelea tukiwa kwenye biashara zetu, hii imetuthibitishia kuwa benki hiyo inatuthamini, na ni ishara thabiti kuwa kauli ya benki hiyo ya stori yako ina thamani kwetu ni ya ukweli kabisa,” alisema.
Siku ya Wapendanao, ambayo hujulikana sana kama Valentine, huadhimishwa tarehe 14 Februari kila mwaka, ambapo hutiwa nakshi na utamaduni maarufu wa wapendanao kupelekeana zawadi za vitu mbalimbali vikiwemo kadi na maua yenye rangi mekundu.
No comments:
Post a Comment