Foreign Exchange Rates

DStv Advert_020324

DStv Advert_020324

SBT Tanzania Advert_291123

Friday 16 April 2021

BENKI YA MAENDELEO YA KILIMO (TADB) NA BENKI YA TAIFA YA BIASHARA (NBC) KUWAWEZESHA MAELFU YA WAKULIMA KUPATA MIKOPO NAFUU

Mkurugenzi wa Fedha wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB), Derick Lugemala (katikati), akizungumza na waandishi wa kabari wakati wa hafla ya kutia saini mikataba kwa ajili ya kuingia makubaliano yakufanya kazi pamoja na Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) yenye lengo la kuwawezesha maelfu ya wakulima wadogo katika minyororo ya thamani ya kilimo. Wengine pichani ni Mkurugenzi wa NBC, Elvis Ndunguru (kushoto) pamoja na Meneja wa Mfuko Maalum wa Dhamana kwa wakulima wadodo kutoka Benki ya TADB,  Asha Tarimo.
Mkurugenzi wa Biashara wa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), Elvis Ndunguru (Kulia), akizungumza na waandishi wa kabari wakati wa hafla ya kutia saini mikataba kwaajili kuingia makubaliano yakufanya kazi pamoja na Benki ya Maendeleo ya kilimo (TADB). Kushoto ni Mkurugenzi wa Fedha wa Benki ya TADB, Derick Lugemala.
Mkurugenzi wa Biashara Benki ya NBC, Elvis Ndunguru (katikati) pamoja na Mkurugenzi wa Fedha wa Benki ya TADB, Derick Lugemala wakitia saini Mikataba ya makubaliano ya kufanya kazi pamoja.
  • Zadhamiria kukuza mitaji na kuleta mageuzi katika kilimo, uvuvi na ufugaji
Dar es Salaam. Jumanne, 13 April, 2021 - Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) imeingia katika makubaliano na benki ya biashara NBC kuwawezesha maelfu ya wakulima wadogo wadogo nchini kupata mikopo yenye riba nafuu ili kuweza kukuza biashara zao na kufanya mageuzi katika sekta ya kilimo, uvuvi na ufugaji.

Makubaliano haya, yaliyosainiwa katika makao makuu ya TADB jijini Dar es Salaam, yataiwezesha benki hiyo kutoa dhamana kwa wakulima watakaoenda kuomba mikopo NBC kufanya shughuli za kilimo, ufugaji pamoja na uvuvi kwa riba nafuu ya asilimia kumi na nne (14%) tu. Dhamana hii inaratibiwa na TADB chini ya mfuko maalum wa dhamana kwa wakulima wadogo nchini ‘SCGS’.

“Kwa muda mrefu tumeona wakulima wetu nchini wakipata changamoto ya mitaji. Wengi wakilazimika kukopa kwa riba za kibiashara ambapo wengi wao wamekuwa wakipata changamoto ya kuhimili riba hizo kubwa. Hivyo, kama taasisi ya maendeleo ya kifedha, kupitia mfuko wa dhamana kwa wakulima wadogo, tumeona umuhimu wa kutoa mikopo hii nafuu kwa kushirikiana na NBC ili kuwawezesha wakulima wengi zaidi kupata mitaji,” alieleza Derick Lugemala, Mkurugenzi wa Fedha kutoka TADB.

Kwa upande wake, Elvis Ndunguru, Mkuu wa Biashara za Kibenki kutoka NBC, alisema kwamba mikopo hiyo watakayokuwa wanatoa kwa dhamana ya TADB itawawezesha kuwakopesha wakulima wadogo mikopo ya mtaji hadi kiwango cha shilingi 50 milioni kwa mkulima mmoja mmoja, shilingi 500 milioni kwa vikundi na vyama vya wakulima, na hadi shilingi 1 bilioni kwa kampuni ambazo miradi yake inawaunganisha na kuwanufaisha wakulima wadogo wengi.

Akieleza vigezo vya kupata mikopo hiyo, Ndunguru alisema:

“Ili kukidhi vigezo vya kupata mikopo hii, mkulima anahitajika kuwa amefanya biashara ya kilimo kwa kipindi kisichopungua miaka mitatu, awe na leseni ya biashara. Awe na kumbukumbu ya taarifa za kifedha. Mikopo hii inapatikana katika matawi yote ya arobaini na saba (47) ya NBC yaliyopo Tanzania bara na Zanzibar. Tunatoa rai kwa wakulima wote wadogo kuchangamkia fursa hii.”

Hapo awali, Lugemala alisema, lengo la mikopo hii yenye masharti nafuu ni kuchagiza benki za kibiashara na taasisi za kifedha kutoa mikopo zaidi kwa wakulima na kuwezesha ukuaji wa minyororo yote ya thamani yanayohusiana na kilimo, uvuvi na ufugaji nchini.

“Mpaka Desemba 2020, mfuko huu wa dhamana ulikwisha toa mikopo katika miradi ya kilimo, uvuvi na ufugaji yenye thamani ya shilingi bilioni 66 na kuwafikia wanufaikaji zaidi ya 9000 moja kwa moja na wasionufaika moja kwa moja 750,000. Baadhi ya miradi tuliyowezesha ni pamoja na kwenye korosho, mpunga, kahawa, miwa, mahindi, mihogo, pamba na ufugaji wa kuku,” alifafanua Lugemala.

Kutokana na taarifa kutoka TADB, mfuko huu wa dhamana ulianzishwa Februari 2018. Na katika kipindi cha miaka mitatu sasa, TADB imeshashirikiana na benki na taasisi za kifedha kama NMB, CRDB, Azania, Benki ya Posta (TPB), Stanbic, FINCA Microfinance, UCHUMI Commercial Bank, Tandahimba Community Bank (TACOBA), Mufindi Community Bank (MUCOBA) na NBC.

“TADB inaamini kwamba kupitia mtandao huu wa ushirikiano wa kimkakati, idadi kubwa ya wakulima wadogo watafikiwa na kuwezeshwa,” alisisitiza Lugemala.

Kuhusu TADB:

Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) ni benki ya umma yenye malengo ya kuongoza mikakati ya kujenga uwezo na mipango ya kuimarisha mnyororo wa thamani wa kilimo na kuunga mkono Serikali ya Tanzania katika kuunda na kutekeleza sera za kilimo na mikopo ya vijijini. Mpaka Desemba 2020, TADB imekwisha nufaisha wakulima 1,788,202 na kutoa mikopo yenye thamani ya shilingi bilioni 300 katika mikoa 26 ya Tanzania Bara na Zanzibar. Mikopo hii imewezesha kukua kwa minyororo ya thamani kwenye sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi.

Kuhusu NBC:

Benki ya NBC ni benki pekee ya kimataifa inayopatikana katika mikoa na maeneo mbalimbali nchini ikiwa na matawi 47 na mashine za ATM zaidi ya 180, pamoja na Mawaka zaidi ya 3,000. Benki ya NBC inatoa huduma mbalimbali za ukusanyaji fedha za huduma nyingine za kibenki kwa wateja mbalimbali kwa zaidi ya miaka 54 nchini . Benki ya NBC sasa imeajiri wafanyakazi takriban 1,100 nchi nzima.

Kwa maelezo zaidi au msaada tupigie +255 76 898 4000/4011 | +255 22 219 3000 | +255 22 551 1000 or email us NBC_Marketingdepartment@nbc.co.tz

Kwa taarifa zaidi:

Amani Nkurlu, Meneja Mahusiano na Masoko – TADB
Barua pepe: amani.nkurlu@tadb.co.tz Simu: +255 754 878 385 au +255 712 223 839


David Raymond, Meneja Mwandamizi-Chapa na Mawasiliano
National Bank of Commerce Limited (NBC)
Barua pepe: david.raymond@nbc.co.tz
Simu: +255 717 742832

No comments:

Post a Comment