Foreign Exchange Rates

DStv Advert_010224

DStv Advert_010224

SBT Tanzania Advert_291123

Friday 23 February 2018

BENKI YA CRDB YAZINDUA TEMBOCARD CREDIT CARDS

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB akionyesha kadi mpya za TemboCard World Reward na Tembocard Gold Credit zilizozinduliwa February 21, 2018 makao makuu ya Benki hiyo jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Charles Kimei (katikati) akizungumza wakati wa uzinduzi wa kadi mpya (TemboCard Word Rewards na TemboCard Gold Credit) uliofanyika makao makuu ya Benki hiyo jijini Dar es Salaam, Februari 21, 2018. Kushoto ni Mkurugenzi wa Huduma Mbadala wa Benki ya CRDB, Philip Alfred na kulia ni Mkurugenzi wa Masoko wa Benki ya CRDB Tully Mwambapa.
Dar Es Salaam Tanzania, February 21, 2018 – Benki ya CRDB kwa kushirikiana MasterCard International wamezindua rasmi kadi mbili zenye mfumo wa “Credit-Card” zijulikanazo kama “TemboCard World Rewards na TemboCard Gold Credit-Card, katika hafla iliyofanyika Makao makuu ya Benki hiyo.

Akizungumza katika uzinduzi huo Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB Dkt. Charles Kimei alisema kadi hizo zenye mfumo wa “Credit-Card” ni za kwanza kuingizwa sokoni na Benki ya CRDB. “Credit-Card ni mfumo maalum wa kadi za kibenki ambapo mteja anaweza kutumia kadi yake kufanya manunuzi au malipo kwa kiwango cha fedha zaidi ya zile alizonazo kwenye akaunti yake” alisema Dkt. Kimei.

Akizungumzia juu ya faida ya kadi hizo Dkt. Kimei alisema zinamuongezea mteja uwezo wa kufanya manunuzi pasipo kuwa na wasiwasi wakutokuwa na fedha za kutosha katika akaunti yake. “Kadi hizi zitamuwezesha mteja kupata mkopo wa muda mfupi na hivyo kumuwezesha kutimiza malengo yake” alisema Dkt. Kimei

Dkt. Kimei alisema TemboCard World Rewards ni maalum kwa ajili ya wateja wakubwa, ambapo mteja atapata mkopo wa hadi shilingi milioni 50, huku muda wa kurudisha mkopo ukifika hadi siku 50. TemboCard Gold Credit Card yenyewe ni maalum kwa ajili ya wateja wa kati na wajasiriamali, ambapo mkopo wao unaenda hadi shilingi milioni 20, na muda wa kurudisha mkopo ukiwa ni siku 45.

“Mbali ya kuwa kadi hizi zinawapa wateja wigo mpana wakufanya manunuzi, wateja pia watakuwa wakinufaika na punguzo la bei katika maduka, hoteli, migahawa na sehemu mbalimbali duniani endapo watafanya malipo kupitia kadi zao, bima ya safari na bidhaa watakazonunua kupitia kadi zao pamoja na fursa ya kutumia zaidi ya kumbi za VIP katika viwanja mbalimbali vya ndege duniani kote” alisema Dkt. Kimei.

Akizungumzia namna ambavyo kadi hizo zitakwenda kusaidia kukuza uchumi wa nchi Dkt. Kimei alisema Credit card zinawezesha watu kufanya malipo ya manunuzi ambayo pengine wasingeweza kumudu kwa wakati huo hivyo kupelekea biashara kuzalisha mapato ambayo kiuhalisia wasingeweza kuyapata, jambo ambalo hupelekea kukua kwa mzunguuko wa fedha na ukuaji wa uchumi kwa ujumla.

Dkt. Kimei alihitimisha hafla hiyo kwa kuwakaribisha wateja wa Benki ya CRDB na watanzania kwa ujumla kutembelea matawi yaliypo karibu yao ilikujaza fomu za maombi ya kupata kadi hizo za “TemboCard World Rewards na TemboCard Gold Credit-Card. “Fomu za maombi pia zinapatikana kupitia website ya Benki, tunawakaribisha hata wale ambao sio wateja bado, tutawafungulia akaunti na kuwapa kadi hizi”, alisema Dkt. Kimei.

Benki ya CRDB ndio Benki ya kwanza kuingiza sokoni kadi yake ya malipo iliyopewa jina la “TemboCard” ambayo kwa kiasi kikubwa imesaidia kuwapa wateja wa Benki hiyo uhuru wa kupata huduma kwa muda na mahali wanapotaka. Tokea ilipoingia sokoni TemboCard imepata umaarufu mkubwa hasa baada ya kuungana na makampuni makubwa yanayotoa huduma za kadi ya Visa, MasterCard na China Union na hivyo kuunda TemboCardVisa, TemboCard MasterCard na hivi karibuni TemboCard China Union Pay.

Kuhusu Benki ya CRDB

Benki ya CRDB ilianzishwa mwaka 1996 na imeendelea kukua zaidi hadi kufikia kuwa benki inayoaminika, chaguo la kwanza la mteja na kuongoza kwa ubanifu katika soko. Benki ya CRDB ina kampuni tanzu tatu (3); CRDB Microfinance inayohusika na kuwahudumia wateja wadogo na CRDB Insurance Brokerage Ltd ambayo hutoa huduma mbalimbali za bima na CRDB Bank Burundi ambayo ni kampuni tanzu ya kwanza nje ya mipaka ya Tanzania, ikiwa ni sehemu ya mpango wa upanuzi wa Benki katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Benki ya CRDB inatoa huduma mbalimbali kwa wateja wakubwa, wakati na wadogo kupitia matawi zaidi ya 255, Matawi yanayo tembea 15, Mashine za kutolea fedha 534, mashine za malipo na manunuzi (PoS) 1,000 na Mawakala wa FahariHuduma 3,000.

Benki ya CRDB Pia hutoa huduma kupitia mtandao yaani “Internet banking” na huduma kupitia simu za mikononi yaani SimBanking.

No comments:

Post a Comment