Foreign Exchange Rates

DStv Advert_010224

DStv Advert_010224

SBT Tanzania Advert_291123

Friday 24 September 2021

BENKI YA BIASHARA YA TANZANIA YABAINISHA MIKAKATI YA KUWAWEZESHA WANAWAKE KIUCHUMI



Benki ya Biashara ya Tanzania (TCB) imedhamiria kuinua hadhi ya wanawake nchini kifedha kwa kuwawezesha kiuchumi na kuwasaidia kuwa wajasiriamali shupavu kupitia mikakati mbalimbali endelevu.

Taasisi hiyo kongwe ya fedha nchini imeweka bayana dhamira hiyo wakati wa Kongamano la Wanawake na Biashara la pili ililoliandaa hapa jana kuwasaidia akinamama kuzing’amua na kuzitumia fursa za kibenki kwa ajili ya maendeleo yao binafsi na taifa kwa ujumla.

TCB imesema itatekeleza jukumu hilo adhimu kwa kuwa kinara wa huduma jumuishi za kifedha za akinamama na kiongozi mbunifu wa huduma hizo sokoni.

Wakiongea kwenye kongamano hilo, maofisa wake waandamizi walisema mafanikio ya jitihada hizo yatatokana na mpango mkakati wa TCB wa kufanya mapinduzi makubwa ya kuwahudumia akinamama.

Aidha, benki hiyo itawaonyesha fursa zinazopatikana TCB na kuwaelimisha jinsi ya kufanya biashara zenye tija. Pia suluhishi za kibenki zilizopo na mpya za kisasa zaidi zitatumika kumkomboa mwanamke kifedha na kumshirikisha kikamilifu katika ujenzi wa taifa.

Wataalamu hao walisema benki hiyo imejiandaa vizuri kwa hilo.Iko imara kifedha, ni uhodari kidijitali na bingwa wa ubunifu ikiwa na wigo mpana wa huduma na mtandao mkubwa wa kuzifikisha popote kwa wakati.

“Tuna mtandao wa matawi makubwa 46, matawi madogo 36, ofisi za wakala za Shirika la Posta Tanzania 120, ATM 84 ambazo zimeunganishwa na ATM 350 za mtandao wa Umoja,” Afisa Mtendaji Mkuu wa TCB, Bw Sabasaba Moshingi alibainisha.

Alisema itakuwa rahisi kuwafikia wanawake wengi na kusaidia kuwawezesha kupitia matawi na vituo vyake vya huduma vilivyosambaa kote Tanzania Bara na Visiwani.

"Pamoja na vikwazo vingi vya kiuchumi wanavyokumbana navyo wanawake na changamoto za kifedha walizonazo, tutahakikisha ajenda ya kuwezesha kiuchumi inafikia malengo yaliyokusudiwa," Bw Moshingi alitabainisha.

"Kupitia makongamano haya, tunataka kubainisha mahitaji maalumu ya kifedha ya akinamama na kuihudumia sehemu hii kubwa ya soko kwa namna ya kipekee,” aliongeza.

Mikutano kama hiyo pia itaandaliwa Zanzibar, Morogoro, Arusha, Mwanza na Dar es Salaam kama jukwaa la kuwakutanisha akinamama kujifunza mambo mbalimbali na kuijua zaidi Benki ya TCB na huduma zake.

Kongamano la Wanawake na Biashara la TCB la ufunguzi lilifanyika mwanzoni mwa mwezi huu jijini Dodoma. La jana lililofunguliwa rasmi na Naibu Spika, Dkt Tulia Ackson, na liliwajumuisha washiriki wapatao 250 waliotumia mijadala ya pamoja kubadilishana uzoefu, kujuana na kujifunza kutoka kwa wajasiriamali waliofanikiwa.

“Lengo kuu la kuwa na utaratibu huu wa makongamano ya akinamama ni kusaidia kuongeza mchango wao katika uchumi wa taifa kupitia fursa mbalimbali hasa zile zinazopatikana TCB,” Bw Moshingi alifafanua katika wasilisho lake.

Kiongozi huyo alitumia takwimu za mafanikio ya TCB kwa kipindi cha mwaka 2007 hadi 2020 kuonyesha uwezo wa kifedha wa benki hiyo kutimiza jukumu hilo.

Mizania ya TCB ilikua kwa zaidi ya asilimia 1,000 hadi takribani TZS trilioni 1.04 huku mikopo ikiongezeka kwa zaidi ya TZS bilioni 580. Hadi sasa akinamama ambao ni nusu ya wateja milioni moja wa TCB wamekopeshwa zaidi ya TZS bilioni 120.

Kuhusu makongamano hayo ambayo mada yake kuu ni “Nafasi ya Mwanamke katika Kukuza Uchumi wa Taifa”, Dkt Ackson alisema yamekuja wakati muafaka na yataisadia serikali kuhakikisha hakuna mwanamke anayeachwa nyuma kiuchumi na kimaendeleo.

"Kupitia mpango huu, TCB itatoa mchango mkubwa katika kubadilisha hadhi ya wanawake nchini kifedha na kiuchumi. Nawapongeza kwa kuja na wazo hili na kuwekeza muda na rasilimali kuhakikisha linafanikiwa," alisema Dk Tulia.

Wachokoza mada ambao wote walikuwa wafanyakazi wanawake wa TCB walisema mikutano hiyo inalenga kuonyesha utayari na uwezo wa benki hiyo kuwasaidia wanawake wajasiriamali.

Walisema TCB inazo fursa lukuki za kibiashara na uwezeshaji kwa ajili yao kupitia huduma maalumu kama akaunti ya Tabasamu na suluhishi mbalimbali kama zile za bima za Nishike Mkono Bima na Kinamama Policy.

No comments:

Post a Comment