Foreign Exchange Rates

DStv Advert_020324

DStv Advert_020324

SBT Tanzania Advert_291123

Wednesday 8 February 2017

MKURUGENZI WA NHC AZINDUA MRADI WA IYUMBU SATELLITE CENTRE ULIOKO MKOANI DODOMA

Mkurugenzi wa Shirika la Nyumba Tanzania NHC Bw. Nehemiah Kyando Mchechu akizungumza na waandishi wa habari wakati alipokuwa akizundua mradi wa uuzaji wa nyumba za Iyumbu mjini Dodoma leo katika mkutano uliofanyika makao makuu wa shirika hilo Upanga jijini Dar es salaam kushoto ni Suzan Omari Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano NHC na kulia ni Pius Tibazarwa Mkurugenzi wa Mauzo na Masoko.

Kama tulivyowaeleza mwaka jana, Shirika la Nyumba la Taifa limetekeleza ahadi yake ya kuunga mkono uamuzi wa serikali wa kuhamia Dodoma kwa kujenga nyumba kwa ajili ya watumishi wa serikali. Kama mnavyofahamu, kwa sasa mji wa Dodoma una mahitaji makubwa ya nyumba kufuatia uamuzi huo wa serikali ya Awamu ya Tano wa kuanza utekelezaji wa kuhamishia shughuli za serikali mjini Dodoma.

Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) leo linazindua rasmi mradi wa kitovu cha mji wa kisasa wa nyumba za gharama nafuu unaotekelezwa eneo la Iyumbu mjini Dodoma. Mradi huu uko jirani kabisa na Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), takriban kilometa kumi kutoka Dodoma mjini. Mradi huu ambao ujenzi wake umeanza Desemba 2016 una ukubwa wa ekari 234 na ni moja ya sehemu ya mji uliopangiliwa kitaalamu kwa kuzingatia sheria na kanuni za mipango miji na utajengwa katika awamu tatu. Ujenzi wa nyumba za awamu ya kwanza utakamilika mwezi Machi 2016.

Awamu hii ya kwanza inahusisha ujenzi wa jumla ya nyumba 300 za gharama nafuu. Nyumba hizi zina ukubwa tofauti tofauti wa mita za mraba 79 zenye nyumba 45, mita za mraba 85 zenye nyumba 210 na mita za mraba 115 zenye vyumba 45. Nyumba zote hizi zina vyumba vitatu kila moja. Ni mradi wa nyumba za chini zisizoungana, maarufu kama stand-alone units. Mradi umesheheni huduma zote muhimu kama vile mfumo wa maji safi na salama, umeme, maegesho ya magari, maji ya akiba, shule ya awali, zahanati pamoja na barabara nzuri zinazopitika.

Vilevile, Shirika la Nyumba la Taifa limetenga, maeneo kwa ajili ya viwanja vya michezo na maeneo ya biashara za maduka ili kuwapatia mahitaji muhimu wakazi wa Iyumbu.

Ili kuwa mmoja wa wamiliki wa nyumba hizi Shirika la Nyumba la Taifa linakukaribisha kuanza kufanya malipo kwa kutumia mifumo mbalimbali ikiwemo kulipia kidogo kidogo (progressive payment plan); au kuchukua mkopo wa nyumba kutoka benki washirika (mortage finance). Hii ni fursa ya pekee kwa Watanzania, wafanyakazi wa Serikali pamoja na taasisi mbalimbali kumiliki nyumba kwenye mradi uliopangwa vizuri wenye mandhari nzuri ya Iyumbu – Dodoma.

Nyumba za awamu hii ya kwanza ya mradi huu zitauzwa kwa bei ya kuanzia TZS 57,670,000.00 bila kodi ya ongezeko la thamani(VAT) mpaka TZS 83,950,000.00 bila kodi ya ongezeko la thamani (VAT). Tunawahamasisha na kuwakaribisha Watanzania wote kufika katika ofisi zetu za Makao Makuu ya Shirika, Ofisi zetu za Mikoa au kupitia baruapepe dg@nhctz.com ili kukamilisha mapema taratibu za manunuzi na kuwa mmoja wa wamiliki halali wa nyumba hizi.

Uzinduzi wa mauzo ya nyumba za mradi huu ni mfululizo wa uzinduzi wa miradi ya nyumba za NHC unaolenga kutimiza malengo ya mkakati wa Shirika wa miaka kumi 2015/16 – 2020/25. Tunatarajia kutekeleza awamu ya pili na ya tatu ya mradi huu ambazo zitahusisha ujenzi wa nyumba kwa ajili ya watu wenye kipato cha kati na juu pamoja majengo makubwa ya shughuli za kibiashara

Ukiwa mdau na mnunuzi mtarajiwa unayehitaji kununua nyumba katika mradi huu, tafadhali waweza tumia akaunti nambari 029103005062 iliyopo National Bank of Commerce(NBC) Tawi la Dodoma au wasiliana na kitengo cha mauzo simu namba 0754 444 333; baruapepe:sales@nhctz.com na pia tembelea tovuti ya Shirika www.nhctz.com kwa maelezo zaidi.

IMETOLEWA NA:
KITENGO CHA MAWASILIANO NA HUDUMA KWA JAMII
SHIRIKA LA NYUMBA LA TAIFA

No comments:

Post a Comment