Blog Rebranding Teaser_030826

Blog Rebranding Teaser_030826

Stanbic Bank Banner_070826

Stanbic Bank Banner_070826

Absa Loan Campaign_160426

Absa Loan Campaign_160426

Wednesday, 5 August 2026

VODACOM TANZANIA YAZINDUA KAMPENI YA "ZAIDI YA MTANDAO" KUKUZA FURSA ZA KIDIJITALI NCHINI

Mkurugenzi wa Biashara na Masoko wa Vodacom Tanzania Plc, Brigita Shirima (katikati), Mkurugenzi wa Vodacom Business, Nguvu Kamando (kulia), pamoja na Kaimu Mkurugenzi wa M-Pesa, Tulisindo Mlupilo (kushoto), wakiwa kwenye picha ya pamoja wakati wa uzinduzi wa kampeni ya "Zaidi ya Mtandao", yenye lengo la kuimarisha dhamira ya Vodacom ya kuleta fursa na huduma zinazozidi mawasiliano kwa wateja wake, kwa kutoa suluhisho halisi zinazoboresha maisha ya kila siku ya jamii. Tukio hilo limefanyika Agosti 4, 2026, katika Makao Makuu ya Vodacom Tanzania Plc, jijini Dar es Salaam.

DAR ES SALAAM, Tanzania; Agosti 4, 2026 – Vodacom Tanzania Plc imezindua rasmi kampeni yake mpya ya "Zaidi ya Mtandao" (More Than a Network), ikisisitiza dhamira yake ya kutoa zaidi ya huduma za mawasiliano kwa kuwezesha fursa za kiuchumi, kijamii na kidijitali kwa Watanzania.

Kampeni hiyo inaonesha mwelekeo wa kampuni wa kuendelea kuwekeza katika teknolojia, ubunifu na suluhisho za kidijitali zinazolenga kuboresha maisha ya wananchi, kusaidia biashara kukua na kuharakisha ujumuishaji wa kidijitali nchini.

Kwa mujibu wa takwimu za Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kwa robo ya mwaka iliyoishia Machi 2026, Vodacom imeendelea kuongoza soko la mawasiliano nchini ikiwa na asilimia 32.3 ya wateja wote, sawa na zaidi ya wateja milioni 36.1.

Aidha, taarifa ya fedha ya kampuni kwa robo ya mwaka iliyoishia Juni 2026 inaonesha kuwa Vodacom imeongeza uwekezaji wake karibu mara mbili ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka uliopita, ambapo uwekezaji ulifikia Shilingi bilioni 123.2. Uwekezaji huo, pamoja na maboresho makubwa ya mfumo wa M-Pesa, unaonesha azma ya kampuni ya kuimarisha ujumuishaji wa kidijitali na kuwawezesha Watanzania wengi zaidi kushiriki katika uchumi wa kidijitali.

Teknolojia Inayozalisha Thamani Halisi

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni hiyo, Mkurugenzi wa Kitengo cha Biashara wa Vodacom Tanzania Plc, Brigita Shirima, alisema kampeni ya Zaidi ya Mtandao ni ahadi ya kuhakikisha teknolojia inaleta matokeo chanya kwa wateja na jamii.

"Zaidi ya Mtandao ni ahadi yetu kwamba teknolojia na huduma tunazotoa lazima zilete matokeo chanya. Iwe ni kumsaidia mwanafunzi kupata elimu ya kidijitali, kuwezesha familia kuendelea kuwa karibu au kusaidia wajasiriamali kukuza biashara zao, tunalenga kuunda fursa zinazoboresha maisha. Kwa sababu mtandao haupimwi kwa teknolojia pekee, bali kwa thamani na fursa unazozalisha kwa watu, biashara na jamii,"alisema Shirima.

Vodacom Business Kuimarisha Mageuzi ya Kidijitali

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Vodacom Business, Nguvu Kamando, alisema biashara za kisasa zinahitaji zaidi ya huduma za mawasiliano, zikihitaji pia suluhisho za kidijitali zinazowawezesha kubuni, kushindana na kukua.

Alisema kupitia Vodacom Business, kampuni inaendelea kuwezesha mashirika, biashara ndogo na za kati pamoja na taasisi mbalimbali kwa huduma za mawasiliano salama, teknolojia za utunzaji wa kumbukumbu, Internet of Things (IoT) na majukwaa ya kidijitali yanayoongeza ufanisi wa biashara.

"Kwetu, 'Zaidi ya Mtandao' kunamaanisha kuwa mshirika wa kuaminika wa kidijitali katika safari ya Tanzania kuelekea Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050," alisema Kamando.

M-Pesa Yaendelea Kuongoza Ujumuishaji wa Kifedha

Naye Kaimu Mkurugenzi wa M-Pesa Vodacom Tanzania Plc, Tulisindo Mlupilo, alisema M-Pesa imeendelea kuwa mhimili muhimu wa ujumuishaji wa kifedha kwa kuwapa mamilioni ya Watanzania huduma za kifedha zinazopatikana kwa urahisi na usalama.

Kwa sasa, mfumo wa M-Pesa unahudumia zaidi ya watumiaji hai milioni 14.1 kila mwezi, kupitia huduma mbalimbali zikiwemo:

  • M-KOBA kwa ajili ya kuweka akiba;
  • SONGESHA kwa huduma za mikopo;
  • M-WEKEZA kwa uwekezaji;
  • LIPA kwa malipo ya biashara; na
  • huduma za kutuma na kupokea fedha kwa urahisi.

Mlupilo alisema maboresho yanayoendelea kufanyika kwenye mfumo wa M-Pesa yataongeza uwezo wa kampuni kutoa huduma za kifedha kwa ufanisi zaidi huku yakichochea maendeleo ya uchumi wa kidijitali nchini.

Zaidi ya Mtandao: Dhamira ya Kuunda Fursa

Vodacom inaamini kuwa thamani ya mtandao haipimwi kwa ukubwa wa wigo wa huduma, kasi ya intaneti au teknolojia pekee, bali kwa fursa na matokeo chanya ambayo mtandao huo unawawezesha watu, biashara na jamii kupata kila siku.

Kadri kampuni inavyoendelea kuwekeza katika miundombinu ya mawasiliano, kuboresha uzoefu wa wateja na kuanzisha suluhisho bunifu za kidijitali, kampeni ya "Zaidi ya Mtandao" itaendelea kuwa msingi wa dhamira ya Vodacom ya kuchochea maendeleo, kuwezesha uchumi wa kidijitali na kuboresha maisha ya Watanzania.


Chanzo: Vodacom Tanzania Plc

Kwa habari zaidi kuhusu sekta ya benki, fedha, teknolojia na biashara nchini Tanzania, endelea kufuatilia Kitomari Banking & Finance Blog kwa habari, uchambuzi na taarifa za uhakika.



No comments:

Post a Comment