Ni katika mkutano wa kwanza wa mwaka wa ulinzi wa faragha ulioandaliwa na PDPC
Dar es Salaam, Tanzania – Juni 30 hadi Julai 1, 2026
Vodacom Tanzania PLC imeonesha uongozi wake katika kuendeleza majadiliano ya kitaifa na kikanda kuhusu ulinzi wa taarifa binafsi, uaminifu wa kidijitali na ubunifu unaowajibika, kupitia ushiriki wake katika Mkutano wa Kwanza wa Mwaka wa Ulinzi wa Taarifa Binafsi uliofanyika jijini Dar es Salaam.
Mkutano huo mkubwa uliwakutanisha wadhibiti wa sekta, viongozi wa taasisi za kifedha, wataalamu wa sheria na wadau wa teknolojia kujadili mustakabali wa usimamizi wa taarifa binafsi katika uchumi unaozidi kuendeshwa kidijitali.
Kuimarisha Usimamizi wa Faragha katika Uchumi wa Kidijitali
Akizungumza katika moja ya majadiliano ya ngazi ya juu, Mkurugenzi wa Sheria wa Vodacom Tanzania PLC, Olaf Mumburi, alishiriki kama mmoja wa wazungumzaji katika mjadala uliolenga ulinzi wa taarifa za kifedha na uchumi wa kidijitali.
Mjadala huo uliwahusisha pia Wakili Dirontsho Mohale kutoka Baakedi Professional Practice (Pty) Ltd ya Afrika Kusini, mwakilishi wa Benki ya Stanbic Tanzania Winston Ishengoma, pamoja na mwakilishi kutoka Benki Kuu ya Tanzania, Abdallah Thabiti.
Washiriki hao walisisitiza umuhimu wa kulinda taarifa za kifedha katika kipindi ambacho huduma za kifedha kidijitali zinaendelea kukua kwa kasi nchini Tanzania na katika ukanda wa Afrika Mashariki.
Nafasi ya Kimkakati ya Maafisa Ulinzi wa Taarifa (DPOs)
Katika mjadala mwingine muhimu uliohusu mada isemayo “Nafasi ya Kimkakati ya Maafisa Ulinzi wa Taarifa (DPOs) katika Kuimarisha Uwajibikaji wa Taasisi na Kujenga Imani katika Uchumi wa Kidijitali,” Mkurugenzi Mtendaji wa Idara ya Taarifa Binafsi wa Vodacom Group Afrika Kusini, David Smuts, alisisitiza umuhimu wa maafisa hao katika kuimarisha uwajibikaji na kujenga uaminifu kwa watumiaji wa huduma za kidijitali.
Alieleza kuwa DPOs si tu wasimamizi wa ufuataji wa sheria, bali pia ni nguzo muhimu katika kujenga imani na kuhakikisha taasisi zinatumia taarifa kwa uwajibikaji.
Mjadala huo pia ulihudhuriwa na:
- Dkt. Doreen Mwamtangala, Mkuu wa Idara ya Sheria na Faragha, Chuo Kikuu Huria cha Tanzania
- Paulo Mwiru, Mkuu wa Uzingatiaji wa Sheria na Utawala, CRDB Bank Plc
- Eng. Steven Wangwe, Mkurugenzi wa Usajili na Uzingatiaji, Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi (PDPC)
Majadiliano hayo yaliangazia umuhimu wa mifumo madhubuti ya udhibiti, uwajibikaji wa taasisi na ushirikiano wa sekta mbalimbali katika kuendeleza mageuzi ya kidijitali.
Ubunifu na Faragha Kuenda Sambamba
Katika mjadala mwingine uliojadili mada isemayo “Je, Ubunifu Unaweza Kustawi Bila Kuhatarisha Faragha?”, Mkuu wa Usalama wa Mtandao wa Vodacom Tanzania PLC, Joel Kazoba, alieleza kuwa ubunifu na ulinzi wa taarifa binafsi lazima viende sambamba.
Alisisitiza kuwa katika uchumi wa sasa wa kidijitali, uaminifu, uwazi na mifumo madhubuti ya ulinzi wa taarifa ni msingi muhimu wa maendeleo endelevu ya teknolojia.
Mjadala huo pia ulihusisha:
- Dirontsho Mohale, Baakedi Professional Practice (Pty) Ltd, Afrika Kusini
- Imani John, Mkurugenzi Mtendaji, Access Bank Tanzania
- Dkt. Nkundwe Mwasaga, Mkurugenzi Mkuu, Tume ya TEHAMA
Kutambuliwa kwa Mchango wa Vodacom
Kushiriki kwa Vodacom Tanzania PLC katika kuendeleza ajenda ya ulinzi wa taarifa kulitambuliwa rasmi wakati wa mkutano huo, ambapo kampuni hiyo ilikabidhiwa tuzo ya shukrani kwa udhamini na mchango wake katika mafanikio ya mkutano huo.
Meneja wa Ulinzi wa Taarifa Binafsi wa Vodacom Tanzania PLC, Upendo Haji, alipokea tuzo hiyo kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi (PDPC), Dkt. Emmanuel Mkilia, kama ishara ya kutambua mchango wa kampuni katika kuendeleza uelewa wa ulinzi wa taarifa nchini.
Viongozi wengine waliokuwepo ni pamoja na wawakilishi wa Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, uongozi wa Bodi ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi, Tume ya TEHAMA na wadau mbalimbali wa kitaifa.
Kujenga Mustakabali Salama wa Kidijitali
Mbali na udhamini, Vodacom Tanzania PLC ilishiriki kikamilifu katika majadiliano yaliyolenga kuimarisha uelewa wa ulinzi wa taarifa binafsi, kuboresha mbinu salama za usimamizi wa taarifa na kukuza ushirikiano kati ya wadau mbalimbali.
Mkutano huo umeweka alama muhimu katika juhudi za Tanzania kuimarisha mifumo ya ulinzi wa taarifa binafsi na kujiweka kama mojawapo ya nchi zinazoongoza katika mageuzi ya kidijitali yanayowajibika na salama.

.jpeg)


No comments:
Post a Comment