Dar es Salaam, 17 Oktoba 2025 – Vodacom Tanzania PLC imetangaza uzinduzi wa filamu ya “NIKO SAWA”, filamu ya kipekee ya Kitanzania inayopatikana kupitia VTV, programu ya kidijitali inayoruhusu watazamaji kufurahia tamthilia na filamu mbalimbali kwa njia ya mtandao.
Hafla ya uzinduzi wa filamu hiyo imefanyika katika ukumbi wa Cinema wa Mlimani City, ikiashiria hatua muhimu katika safari ya Vodacom ya kuwaunganisha Watanzania kupitia teknolojia. Kupitia ubunifu huu, kampuni inalenga kuchochea mazungumzo kuhusu masuala nyeti ya kijamii kwa kutumia burudani kama chombo cha elimu na uhamasishaji.
Filamu ya “NIKO SAWA” inaangazia kwa kina mada ya afya ya akili — eneo ambalo kwa muda mrefu limepuuzwa katika jamii. Ikiandikwa na kuongozwa na watayarishaji wabunifu wa Kitanzania, filamu hii inasimulia hadithi ya familia inayopambana na changamoto za kifedha, msongo wa mawazo na mapambano ya kimya kimya yanayoathiri maisha ya kila siku.
Filamu hii imezinduliwa sambamba na maadhimisho ya Mwezi wa Uhamasishaji wa Afya ya Akili, ikiweka msisitizo juu ya umuhimu wa kuelewa na kujali hali za watu wanaotuzunguka.
Akizungumza wakati wa uzinduzi, Goodluck Moshi, Mkuu wa Idara ya Ubunifu wa Kidijitali wa Vodacom Tanzania, alisema kuwa kupitia VTV, lengo la kampuni si kuburudisha tu bali pia kuwezesha jamii.
“NIKO SAWA ni hadithi inayogusa maisha na hisia za watazamaji, hususan vijana, ikikumbusha kwamba afya ya akili ni muhimu sawa na afya ya mwili. Tunaamini teknolojia na sanaa ya usimulizi zinaweza kushirikiana kuleta mazungumzo ya kweli na kuijenga jamii yenye huruma na mshikamano,” alisema Moshi.
Kwa upande wake, Neema Ndepanya, muongozaji wa filamu hiyo, alieleza kuwa hadithi hiyo imetoka moyoni na inalenga kuzungumzia maumivu ya kimya kimya ambayo watu wengi hubeba kila siku.
“Kufanya kazi na Vodacom na kushuhudia NIKO SAWA ikipata uhai kupitia VTV imekuwa safari ya maana na yenye kugusa hisia. Pale ambapo taasisi kama Vodacom zinawekeza katika hadithi za ndani, zinasaidia si tu sanaa bali pia kuponya jamii, kuanzisha mazungumzo na kutoa matumaini kwa wale wanaoyahitaji zaidi,”aliongeza Neema.
Wateja wanaweza kufurahia maudhui ya VTV kwa kupakua bure programu ya VTV OTT kupitia Play Store au App Store. Baada ya kujisajili, watazamaji wanaweza kuchagua kifurushi cha bei nafuu kuanzia TZS 500 pekee, na kufanya malipo kwa urahisi kupitia M-Pesa au njia nyingine za malipo ya simu. Pia, kuna ofa maalum na muda wa ziada wa kutazama.
Uzinduzi wa “NIKO SAWA” unaashiria hatua nyingine muhimu katika dhamira ya Vodacom ya kujenga maisha ya kidijitali yenye maana kwa Watanzania — maisha yanayowawezesha, kuwaburudisha na kuwaunganisha katika matukio na hisia halisi za maisha ya kila siku.

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)

No comments:
Post a Comment