Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu (Mb), ameishukuru Marekani kupitia Shirika lake la Changamoto za Milenia (Millennium Challenge Corporation-MCC) kwa kuiteua Tanzania kuwa moja ya nchi zilizoko kwenye mpango wa kunufaika na ruzuku zinazolenga kusaidia mageuzi ya kisera na kitaasisi ili kutatua vikwazo vya ukuaji uchumi.
“Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameituliza nchi kisiasa, na kuwa na nia ya dhati ya kuituliza nchi kwa kuruhusu masuala ya kisiasa kufanyika kwa uwazi na hata hii si tu kwa ajili ya kutekeleza vigezo vya taasisi yoyote bali ni nia yake ya dhati ya kulinda uhuru wa watu” alisema Dkt. Nchemba.
Kwa upande wake, Naibu Afisa Mtendaji Mkuu wa Shirika la Changamoto za Milenia (MCC), Bi. Chidi Blyeden, ameipongeza Tanzania kwa hatua kubwa ilizopiga katika kuimarisha masuala ya utawala bora, demokrasia na haki za binadamu chini ya utawala wa Dkt. Samia Suluhu Hassan, hatua iliyolifanya Shirika lake kurejesha ushirikiano na Serikali.
Bi. Blyeden alieleza kuwa Wataalam kutoka MCC wanaendelea na mijadala na wataalam wa Serikali ili kuharakisha kuanza kwa utekelezaji wa mpango huo ambao matokeo yake hapo baadae utaiwezesha Marekani kurejesha mradi wa Changamoto za Milenia (MCC-Compact) ambao utakuwa na lengo la kusaidia nchi kutekeleza miradi mikubwa ya kimkakati ya maendeleo.
Mwezi Desemba mwaka 2023, Bodi ya Shirika la Changamoto za Milenia (MCC), ilizichagua Tanzania na Philippines, kama wabia wake katika kuandaa programu za awali (threshold programs) zitakazolenga katika mageuzi ya kisera na kitaasisi ambazo nchi hizi zinaweza kuyafanya ili kupunguza umasikini na kuchochea ukuaji wa uchumi.
Bodi hiyo ya MCC ilichukua uamuzi huo baada ya Tanzania na Ufilipino, kuonesha dhamira mpya ya kusukuma mbele mageuzi muhimu ya kuimarisha utawala wa kidemokrasia, kulinda haki za binadamu na kupambana na rushwa.
Shirika la Changamoto za Milenia (MCC), ni shirika huru la Serikali ya Marekani linalojielekeza kupunguza umaskini duniani kupitia ukuaji wa kiuchumi, kwa kutoa ruzuku na misaada ya muda maalum kwa nchi zinazokidhi viwango na vigezo thabiti vya utawala bora, mapambano dhidi ya rushwa na kuheshimu haki za kidemokrasia.
No comments:
Post a Comment