Na Mwandishi Wetu – Dar es Salaam
04 Julai 2025
Katika kuendeleza dhamira yake ya kuimarisha uwazi, uwajibikaji, na uchumi jumuishi, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), kwa kushirikiana na SICPA Tanzania, inaendelea kuelimisha umma kuhusu nafasi ya teknolojia katika kulinda walaji, kuhakikisha ulipaji sahihi wa kodi, na kulinda uchumi wa Taifa.
Kukabiliana na Bidhaa Bandia kwa Teknolojia ya Kisasa
Katika mazingira ya biashara yanayobadilika kwa kasi, Watanzania wanakabiliwa na changamoto ya bidhaa bandia na biashara haramu ambazo si tu kwamba zinahatarisha afya na usalama wa walaji, bali pia zinapunguza mapato ya serikali yanayotumika kufadhili huduma muhimu za jamii.
TRA, kupitia majukwaa kama Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba), inatumia fursa hii kuelimisha wananchi juu ya njia rahisi za kuchangia mapambano dhidi ya bidhaa bandia na kuunga mkono maendeleo ya Taifa.
Wananchi Wanapata Nini?
Katika ushiriki wake kwenye Sabasaba, TRA inawawezesha wananchi kwa kutoa:
- Maarifa kuhusu mfumo wa kisasa wa Stempu za Kodi za Kielektroniki (ETS) – unaosaidia kutambua bidhaa halali kwa urahisi na kuwalinda walaji dhidi ya bidhaa hatarishi.
- Mafunzo ya vitendo ya kutumia programu ya Hakiki Stempu – programu ya simu janja inayowawezesha watumiaji kuthibitisha uhalali wa bidhaa kama vinywaji, vileo na sigara kwa sekunde chache.
- Uelewa wa uhusiano kati ya kodi na maendeleo ya Taifa – ikielezwa wazi kuwa kila bidhaa halali inayonunuliwa huchangia ujenzi wa shule, hospitali, barabara, na huduma nyingine muhimu.