Singida – Julai 10, 2025
Mkuu wa Kanda ya Kati wa Vodacom Tanzania, Chiha Nchimbi (kulia), pamoja na Mkuu wa Mtandao wa Matawi wa Benki ya Stanbic Tanzania, Geofrey Mwijage (kushoto), wamekabidhi miche 100 ya miti kwa Mkuu wa Divisheni ya Awali na Msingi wa Manispaa ya Singida, Omari Maje, katika Shule ya Msingi Minga, mkoani Singida.
Hafla hiyo imefanyika ikiwa ni sehemu ya msafara wa Twende Butiama, unaoendelea nchini na uliozinduliwa rasmi mnamo Julai 3, 2025.
Mbali na miche hiyo ya miti, msafara huo pia umetoa msaada wa magodoro 30, vitanda 5, mashuka 20, madawati 10, pamoja na vitimwendo 6 (wheelchairs) kwa wanafunzi wenye uhitaji maalum katika shule hiyo.
Kwa pamoja, Vodacom Tanzania na Benki ya Stanbic Tanzania wanadhamini msafara huu, ambao umebeba ujumbe wa kuhimiza uzalendo, mshikamano na kusaidia jamii kupitia shughuli mbalimbali za kijamii na mazingira.
"Tunaamini kuwa kusaidia shule zetu na mazingira ya kujifunzia ni msingi wa kujenga taifa lenye elimu bora na kizazi chenye maadili. Kupitia msafara huu, tutaendelea kutoa msaada na kugusa maisha ya Watanzania wengi zaidi," alisema Chiha Nchimbi wa Vodacom.
Kwa upande wake, Geofrey Mwijage alisisitiza dhamira ya Stanbic katika kuwa mshirika wa maendeleo endelevu kwa Watanzania:
“Tunajivunia kushirikiana na Vodacom katika kuleta mabadiliko chanya kwenye jamii. Uwekezaji katika elimu na ustawi wa watoto ni sehemu ya mkakati wetu wa kuwainua wananchi kiuchumi na kijamii.”
Msafara wa Twende Butiama utaendelea katika mikoa mbalimbali nchini, ukiambatana na shughuli za kijamii, michezo, na elimu kwa jamii, ikiwa ni kumbukizi ya historia na maono ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.
No comments:
Post a Comment