Dar es Salaam, Tanzania — 15 Oktoba 2025:
Vodacom Tanzania PLC, kwa ushirikiano na Bolt, kampuni inayoongoza katika huduma za usafiri kwa njia ya mtandao, wamezindua huduma mpya inayowawezesha wateja kupata thamani zaidi katika kila safari wanayofanya. Kupitia mpango wa Tuzo Points, wateja wa Vodacom sasa wanaweza kutumia pointi walizopata kupata punguzo la bei kwenye safari za Bolt — wakileta pamoja nguvu ya teknolojia, urahisi wa usafiri, na maisha ya kila siku yenye thamani zaidi.
“Dhamira yetu Vodacom daima imekuwa kuwaunganisha Watanzania kwa ajili ya mustakabali bora,” alisema Joseph Njuu, Meneja wa Usimamizi wa Thamani ya Wateja, Vodacom Tanzania.
“Ushirikiano huu na Bolt ni uthibitisho wa dhamira hiyo — tunaleta suluhisho rahisi linalowawezesha wateja na kuwazawadia kwa safari zao za kila siku.”
Kupitia ushirikiano huu, wateja wa Vodacom sasa wanaweza kutumia Tuzo Points ambazo hapo awali zilitumika kupata muda wa maongezi au bando za intaneti, kulipia safari za Bolt kwa punguzo maalum. Huduma hii ni rahisi kutumia, ya kisasa, na imeundwa mahsusi kwa ajili ya Mtanzania wa leo anayethamini urahisi, uunganisho, na thamani katika maisha yake ya kila siku.
Milu Kipimo, Meneja wa Nchi wa Bolt Business kwa Tanzania, Ghana na Afrika Kusini, alisema:
“Kushirikiana na Vodacom kunafungua milango zaidi ya fursa za kiuchumi na masoko. Kwa kuunganisha nguvu za kampuni inayoongoza katika mawasiliano nchini na jukwaa linaloongoza katika huduma za usafiri, tutawezesha wakazi wa mijini, wajasiriamali, na wataalamu kuongeza tija katika kazi zao jambo litakalochochea ukuaji wa uchumi.”
Wateja wa Vodacom hupata Tuzo Points kiotomatiki kila wanapoongeza bando au kufanya miamala kupitia M-Pesa. Pointi hizo zinaweza kuonekana kupitia M-Pesa App au kwa kupiga *149*01#.
Ili kutumia pointi hizo kupata punguzo kwenye safari za Bolt, mteja atachagua chaguo la “Tumia Tuzo Points kwa Bolt”, na kupokea nambari ya punguzo (promo code) ya kuingiza kwenye Bolt App wakati wa malipo.
Kadri Vodacom inavyoendelea kusherehekea miaka 25 ya kuwaunganisha Watanzania, ushirikiano huu na Bolt unaendeleza dhamira yake ya kujenga jamii iliyounganishwa na kuboreshwa kupitia teknolojia — jamii ambayo maisha yake yanazidi kuwa bora kutokana na ubunifu.


.jpeg)
.jpeg)
No comments:
Post a Comment